Waziri Lukuvi aagiza Halmashauri Kutoa vibali vya ujenzi vitolewe ndani ya siku tatu


Halmashauri nchini zimeagizwa kuanza kutoa vibali vya ujenzi ndani ya siku tatu, huku maofisa mipango miji wakitakiwa kusimamia agizo hilo

Pia, imesisitiza kuwa kazi ya urasimishaji maeneo yaliyojengwa kiholela lazima iendelee na haitakiwi kuambatana na ubomoaji wa nyumba za watu

Maagizo hayo yalitolewa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi alipokuwa akifungua mkutano wa Bodi ya Wataalamu wa Usajili Mipango Miji jijini Dodoma jana

Lukuvi alisema vibali vya ujenzi wa nyumba katika maeneo mbalimbali nchini ni lazima vitolewe ama katika maeneo yaliyopangwa au yasiyopangwa na kwamba, jambo la msingi inalotaka Serikali ni kuwa na majengo yaliyopangiliwa vizuri. “Ucheleweshwaji wowote wa utoaji kibali lazima mhusika afahamishwe sababu,” alisema Lukuvi

Alisema lengo la maofisa mipango miji kupewa mamlaka ya kutoa vibali vya ujenzi badala ya wakuu wa idara wa halmashauri linatokana na baadhi ya maeneo hayo kusimamiwa na watu wasiokuwa na taaluma ya sekta husika, jambo linaloweza kuvuruga upangaji wa miji

Waziri Lukuvi alitaka nakala za vibali vya ujenzi zitakazotolewa zipelekwe pia katika ofisi za maofisa watendaji wa mitaa kwa kuwa wanapaswa kufahamu kinachoendelea katika maeneo yao. Pia, aliagiza bodi za usajili wa mipango miji kuandaa mwongozo utakaowasaidia watendaji wa mitaa kuwa na ufahamu katika kusimamia mipango ya uendelezaji miji, jambo litakalosaidia kuepuka ujenzi holela kwa baadhi ya maeneo

Kuhusu urasimishaji maeneo yasiyopimwa, alisema licha ya kazi hiyo kufanyika nchi nzima, hakuna nyumba itakayovunjwa na kutaka kampuni zote zitakazotaka kufanya kazi ya urasimishaji ardhi kutuma maombi kupitia ofisi za wilaya

Akizungumza katika mkutano huo, mtafiti na mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Ardhi (Aru), Salfonce Kesi alisema kwa sasa mambo mengi ya upangaji miji nchini hayaendi vizuri kutokana na mipango kufanywa na watu wasio na taaluma hiyo. Kesi alisema lazima suala la mipango miji katika maeneo lianze na mipango mingine ya huduma za jamii

Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Mipango Miji, Profesa Wilbert Kombe alisema wameanza kuchukua hatua kuhakikisha taaluma ya mipango miji inakuwa na wataalamu wanaozingatia sheria

Waziri Lukuvi aagiza Halmashauri Kutoa vibali vya ujenzi vitolewe ndani ya siku tatu Waziri Lukuvi aagiza Halmashauri Kutoa vibali vya ujenzi vitolewe ndani ya siku tatu Reviewed by KUSAGANEWS on October 31, 2018 Rating: 5

No comments: