CCM Simanjiro wamkaribisha Millya

Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara, Awadhi Omary amemkaribisha aliyekuwa mbunge Simanjiro (Chadema), James Millya ndani ya chama hicho tawala

Akizungumza leo jioni Jumapili Oktoba 7, 2018, Awadhi amesema hatua hiyo ni faraja kwa CCM hivyo wanamkaribisha kwa mikono miwili kwani jimbo hilo halitakuwa kwenye mikono ya Chadema tena

Amesema ni jambo la heri kuona mtu akikimbia kwake anakuja kwako endapo atakuja kwa nia nzuri ni furaha kubwa kwako

"Hata hivyo, suala la kugombea ubunge wa Simanjiro litasubiri vikao halali juu ya Millya endapo atapitishwa au laa," amesema Awadhi

Diwani wa Endiamtu (Chadema), Philemoni Oyogo amesema amesikitishwa mara baada ya kupata taarifa kuwa Millya amejiuzulu nafasi hiyo na amehamia CCM

Oyogo amesema yeye ataendelea kuwa diwani wa Endiamtu kupitia Chadema na hayupo tayari kujiuzulu nafasi hiyo na kujiunga na CCM

Diwani wa Mirerani (Chadema), Thomas Yohana amesema hawezi kuzungumza chochote zaidi kwani Millya ametumia demokrasia yake kama Mtanzania kujiunga CCM

"Siwezi kuzungumza chochote yeye ametumia uamuzi wake ila mimi siwezi kuhama Chadema eti kwa sababu ya kumuunga mkono yeyote nitaendelea kuwa diwani wa Mirerani kwa tiketi ya Chadema," amesema Yohana

Hata hivyo, baadhi ya wananchi wa wilaya ya Simanjiro wamepongeza hatua ya Ole Millya kuondoka Chadema na kujiunga na CCM

Mkazi wa mtaa wa Kazamoyo, Mustafa Kabota amesema Millya alienda Chadema kwa ajili ya kutafuta mabadiliko lakini amerudi baada ya kuona hakuna mabadiliko yoyote na kuamua kurudi CCM

"Nawaomba madiwani wa kata ya Mirerani na Endiamtu ambao nao wapo Chadema warudi CCM kwani huko Chadema hakuna wanachokifanya," amesema Kabota

Mkazi wa Mirerani, Hassan Juma amesema hata ukuta unaozunguka migodi ya madini ya Tanzanite uliwekwa ili kuwakomoa wananchi wa eneo hilo baada ya kumchagua Millya na madiwani wa Mirerani na Endiamtu

"Nadhani sasa hivi tutaruhusiwa kupita ndani ya ukuta kwani haya mambo ya kisiasa yalitugharimu ila kwa sababu jamaa amemuunga mkono mzee sasa mambo yatakuwa safi," amesema Juma

Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Manyara, Gervas Sulle amesema hana taarifa ya Millya kujiuzulu ubunge na kuhamia CCM

"Sina hizo taarifa rasmi za Millya ila Katiba inamruhusu ni uhuru wa mtu hao wanaosema tumepata pigo hakuna pigo tulilolipata," amesema Sulle

Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, Millya alimshinda mkuu wa Mkoa wa Njombe Christopher Ole Sendeka na pia madiwani sita wa Chadema walishinda kwenye kata za Mirerani, Endiamtu, Naberera, Loiborseret, Ruvu Remit na Loiborsoit

Katika mkoa wa Manyara Chadema ilishinda majimbo mawili ya Simanjiro na Babati Mjini linaoongozwa na Pauline Gekul wa Chadema kati ya majimbo saba



CCM Simanjiro wamkaribisha Millya CCM Simanjiro wamkaribisha Millya Reviewed by KUSAGANEWS on October 07, 2018 Rating: 5

No comments: