Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- Tawala za Mikoa na Serikali
za Mitaa Selemani Jafo amewataka Wakuu wapya wa Wilaya walioteuliwa hivi
karibuni kuacha tabia ya kutumia vibaya mamlaka waliyonayo na kuwaweka rumande
wananchi pamoja na watumishi wa umma hali inayopelekea kuichukia serikali yao.
Mhe. Jafo aliyasema hayo leo Jijini Dodoma kwenye kikao kazi
na Wakuu hao wa wilaya kwa lengo la kuwapa maelekezo ya kazi ambapo mada kuu ya
kikao hicho ni mahusiano na mawasiliano kazini pamoja na kuhakikisha kuwa
wanafanya kazi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo
“Msiende kuwa vyanzo vya migogoro kwenye Wilaya zenu,
tumekuwa tukishuhudia migogoro baina ya Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi, Wenyeviti
wa Halmashauri, Makatibu Tawala pamoja na Wabunge, hatuwezi kwenda hivi,
katengenezeni serikali” Alisema Waziri Jafo
Aidha aliwataka Wakuu hao wapya wa Wilaya kutoa ushirikiano
kwa wale wanaotekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na siyo vinginevyo
ikiwa ni pamoja kusimamia miradi ya maendeleo ikiwemo uboreshaji wa miundombinu
ya afya na elimu unaoendelea kote nchini
Naye Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Injinia Mussa
Iyombe amewataka Wakuu hao wa wilaya kuzitendea haki nafasi walizopewa kwa
kufanya kazi kwa kuzingatia sheria, taratibu na kanuni zilizopo hasa pale
wanapomuadhibu mtumishi aliyekosea.
“Serikali ina taratibu zake, baadhi ya wakuu wa wilaya
walikuwa wanatia aibu, kama kuna mtumishi kakosea, tumia mamlaka zinazomuongoza
kumshughulikia, na sio kusimamisha watu kazi hovyo, kutumbua tumbua hovyo”
Alisisitiza Injinia Iyombe
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Jerry Muro
amesema watahakikisha wanafanya kazi kwa kuzingatia kasi ya Rais Dkt John Pombe
Magufuli
Naye Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe Jokate Mwegelo amesema ni
muda wa kufanya kazi na sio kuongea ongea sana huku akiahidi kufuata miongozo
iliyotolewa na viongozi wa juu kwenye utekelezaji wa majukumu yake
Madc waonywa Kutumia Vibaya Madaraka Yao
Reviewed by KUSAGANEWS
on
August 15, 2018
Rating:
No comments:
Post a Comment