Wadau wa masuala ya habari na wanasheria wamepinga kauli ya
Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Simon Sirro kwamba mwanahabari Silas Mbise
alishambuliwa na polisi kwa kutotii sheria
Sirro aliyasema hayo jana jijini Arusha wakati akizungumza
na vyombo vya habari baada ya kuulizwa juu ya hatua za uchunguzi wa jalada
lililofunguliwa polisi la kupigwa kwa mwandishi huyo wa Wapo Redio katika
Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, Agosti 8
“Taarifa za awali tulizonazo ni kwamba mwandishi huyo
alikuwa mbishi katika kutii agizo la askari aliyemkataza kuingia sehemu ambayo
walizuiliwa hadi kufikia kumkaba askari akilazimisha kuingia ndipo askari naye
akapata hasira wakafikia hali hiyo,” alisema IGP Sirro akizungumzia tukio hilo
lililotokea siku maalumu ya Klabu ya Simba (Simba Day)
Alisema uchunguzi wa tukio hilo bado unaendelea na baadaye
polisi itaeleza ukweli na hatua za kisheria zitafuata dhidi ya atakayebainika
kutenda kosa
“Ngoja tuone upelelezi na ushahidi utasemaje, ukimalizika na
kama kuna aliyemuonea mwenzake hatua za kisheria zitafuata hivyo kama askari
alimpiga kwa kumuonea atachukuliwa hatua za kisheria na kama mwandishi naye
alifanya fujo huko na kukimbilia kwenye kamera aonekane tutamchukulia hatua pia
maana hakuna aliye juu ya sheria,” alisema
Sirro pia alitumia nafasi hiyo kuwataka waandishi kufanya
kazi zao vyema kwa kutii mamlaka na sheria zilizopo ili kufanya kazi zao kwa
weledi
Agosti 9, ikiwa ni siku moja baada ya Mbise kupigwa, Msemaji
wa Jeshi la Polisi, Barnabas Mwakalukwa alisema IGP Sirro ameagiza kufunguliwa
kwa majalada mawili, likiwemo la malalamiko ya Mbise ya kupigwa na la kuangalia
maelezo ya polisi kuwa Mbise hakutii sheria.
Baada ya kauli ya
Sirro jana, wadau wa habari na wanasheria walisema mkuu huyo wa polisi ametoa
hukumu wakati bado uchunguzi wa suala hilo haujakamilika
Walisema kauli yake haiwezi kutoa haki kwa mwandishi wa
habari aliyepigwa
Akizungumza na Mwananchi, Kaimu Mwenyekiti wa Jukwaa la
Wahariri nchini (Tef), Jesse Kwayu alisema video zilizorekodiwa zinaonyesha
mwandishi akipigwa na polisi akiwa hana silaha, amelala chini na kuinua mikono
juu
Alisema huo ni mfululizo wa matukio ya jeshi hilo
kuwanyanyasa raia
“Kauli ya IGP ni ya kusikitisha, its unfortunate statement
(ni kauli ya kusikitisha). Asimamie sheria na weledi wa polisi katika
kutekeleza majukumu yao ya kulinda usalama wa raia na mali zao,” alisema Kwayu
Pia alihoji ni sehemu gani ambayo mwandishi wa habari
haruhusiwi kuingia akiwa katika uwanja huo kama IGP Sirro alivyoeleza
Alisema mkuu huyo wa polisi anajaribu kufukia maovu ya jeshi
hilo badala ya kukemea
Akiwa na mtazamo kama huo, Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa
Haki za Binadamu (THRDC), Onesmo Olengurumwa alipendekeza kuwepo chombo
kitakachosimamia malalamiko yote dhidi ya Jeshi la Polisi
Olengurumwa alisema alitarajia kusikia IGP akikemea suala
hilo kama walivyofanya mawaziri, lakini ameanza kuwakingia kifua askari
waliohusika kwenye unyanyasaji huo kabla hata uchunguzi haujakamilika
“Kitendo cha yeye kutoa tamko kabla hata uchunguzi haujakamilika
inaonyesha dhamira yake ya kutaka kuwalinda askari wake. Ifike mahali tuwe na
chombo huru ambacho kitasimamia malalamiko ya matukio ambayo Jeshi la Polisi
linahusika,” alisema
Mwanasheria na Rais mstaafu wa Chama cha Wanasheria cha
Tanganyika (TLS), John Seka alisema kauli ya mkuu wa polisi inawaaminisha watu
kwamba askari hawakufanya kosa kumshambulia mwandishi huyo
Alisema video inaonyesha askari wakimshambulia raia ambaye
alikuwa haonyeshi upinzani wowote
Seka alisema kuwa hata kama mwandishi huyo alileta upinzani,
ilifikia hatua akasalimu amri kama ilivyoonekana, lakini bado waliendelea
kumpiga. “Kuna haja ya askari wetu kufanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia
sheria, kanuni na maadili ya kazi yao. Msimamizi wa mkuu wa taratibu hizo ni
IGP Sirro, ninatumaini watatenda haki kwa mwandishi wa habari,” alisema
Kauli ya IGP Sirro Kuhusu Kupigwa Mwanahabari Yaanza Kutibua Mapya
Reviewed by KUSAGANEWS
on
August 17, 2018
Rating:
No comments:
Post a Comment