Fred Lowassa azungumzia kilichotokea Monduli, ataka maridhiano kitaifa


Dar es Salaam. Fred, mtoto wa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, ameelezea kilichotokea Monduli katika mchakato wa kumpata mgombea ubunge wa jimbo hilo akisema, “Sikuwahi kuchukua fomu na ninaiheshimu sana Chadema.”

Fred ametoa kauli hiyo kipindi ambacho jina lake limekuwa kwenye mijadala ndani na nje ya Chadema kwamba, alijitokeza kuchukua fomu ya kuwania ubunge wa jimbo hilo lililoongozwa na baba yake (Lowassa) kwa miaka 20

Lowassa alikuwa mbunge wa Monduli kati ya 1995-2015. Uchaguzi wa ubunge katika majimbo matatu likiwamo la Monduli na udiwani wa kata 21 utafanyika Septemba 16, baada ya wabunge wawili kuhama Chadema na kwenda CCM huku aliyekuwa mbunge wa Korogwe Vijijini (CCM), Stephen Ngonyani ‘Profesa Majimarefu’ akifariki dunia Julai 2

Waliotimkia CCM ni Mwita Waitara (Ukonga) na Julius Kalanga (Monduli) ambao Kamati Kuu ya CCM imewapitisha kugombea tena ubunge pamoja na Timotheo Mzava anayewania Korogwe Vijijini

Wakati CCM ikiwapata wagombea kwenye majimbo hayo, Chadema imewapitisha Asia Msangi (Ukonga) na Amina Saguti kuwania Korogwe Vijijini, huku Monduli akiwa ni Yonas Laizer ambapo kampeni za uchaguzi huo zinaanza Agosti 21

Jana, Mwananchi lilizungumza na Fred kujua kilichojiri hadi kujitoa kwake ambapo alisema, “Nawaheshimu sana sana Chadema, walitupa heshima kubwa sana mwaka 2015 kwa mzee (Lowassa) kuwa mgombea na wana CCM waliojiunga na mabadiliko nao kupewa fursa ya kugombea.”
Katika uchaguzi wa mwaka huo, Lowassa na Ukawa walitoa changamoto kwa mgombea wa CCM, Dk John Magufuli, ambapo mgombea huyo wa Ukawa alipata kura 6,072,848, huku Dk Magufuli akitagazwa mshindi kwa kupata kura 8,882,935

Fred ambaye ni mtoto wa kwanza kati ya watano wa Lowassa na mkewe, Regina alipoulizwa kama fomu alichukua ya kugombea Monduli, alisema, “Fomu sijawahi kuchukua (ingawa) nia ya kutaka kushiriki uongozi Monduli ninayo lakini si sasa.”

Alikiri kuwapo kwa ushawishi kutoka kwa wanachama wa Chadema lakini aliona siyo wakati wake

Alisema yeye na familia watamuunga mkono mgombea mwenye nguvu ya mabadiliko atakayepitishwa

“(Lakini) alichofanya ndugu yetu Kalanga, amekosa fadhila kwa wana Monduli, nasikitika tunaingia katika uchaguzi mdogo kwa mtu aliyekosa fadhira.”

Fred alisema Monduli inatizamwa kwa jicho la kipekee kutokana na kuwa na wilaya iliyotoa mawaziri wakuu wawili ambao ni Lowassa na Hayati Edward Sokoine ambao makazi yao hayaachani hata kilomita mbili

“Mgombea wa ‘spirit’ (nguvu) ya mabadiliko nitamuunga mkono,” alisema Fred huku akisisitiza kwamba familia ya Lowassa itaendelea kutoa huduma kwa wana Monduli. “Familia ya Lowassa siku zote itaendelea kuwa watumishi kwa jamii ya Monduli bila cheo chochote.”

Alipoulizwa juu ya mtazamo wake wa chaguzi za hivi karibuni, Fred alisema Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) inapaswa kuyafanyia kazi malalamiko yanayotolewa

“Nchi kubwa kama Marekani wanaongea, (hivyo) kuna jambo la kutafakari kwa nini wameongea,” alisema Fred akizungumzia kauli iliyotolewa na Ubalozi wa Marekani nchini. Nakubaliana na (Kabwe) Zitto (kiongozi wa ACT-Wazalendo) kwamba ni muda muafaka kufanya mkutano wa kitaifa wa maridhiano ya kisiasa.”

Hivi karibuni, Zitto ambaye ni mbunge wa Kigoma Mjini alisema kutokana na hali ilivyo nchini, umefika wakati ufanyike mkutano wa maridhiano ya kisiasa ili kurejesha kuaminiana na kusonga mbele kama Taifa

Fred Lowassa azungumzia kilichotokea Monduli, ataka maridhiano kitaifa Fred Lowassa azungumzia kilichotokea Monduli, ataka maridhiano kitaifa Reviewed by KUSAGANEWS on August 18, 2018 Rating: 5

No comments: