Wakati CCM ikitaja siri ya ushindi wao katika kata 77 na
ubunge wa Buyungu, Chadema imekosoa mwenendo wa uchaguzi huo mdogo, ikilia na
vyombo vya dola kutowatendea haki
Katibu mkuu wa Chadema, Dk Vincent Mashinji alisema jana
kuwa vyombo vya dola vilitumia nguvu kubwa kuhalalisha ushindi wa CCM
CCM imeshinda katika kata zote 77 ambapo kati ya hizo, 41
walipita bila kupingwa, huku pia mgombea wao Christopher Chiza akishinda ubunge
katika Jimbo la Buyungu mkoani Kigoma
Akijibu swali baada ya kuulizwa wamekwama wapi na kukosa
ushindi katika maeneo yote, Dk Mashinji alisema, “sisi hatujakwama, utaratibu
umeenda vizuri, kampeni zilifanyika vizuri na watu walijitokeza kwa wingi
kupiga kura lakini baada ya kuona matokeo kwamba tumeshinda, vyombo vya dola
vimeamua kuvuruga.”
Dk Mashinji alisema wananchi wanapaswa kujua kwamba chaguzi
zimekuwa zikiingiliwa
“Tume ya Uchaguzi siyo huru unadhani hapo haki itatekelezwa?
Ndiyo maana vyombo vya dola vinapoingilia mchakato hakuna cha kufanya,” alisema
Alikwenda mbali zaidi na kusema kuwa umefika wakati wa
wananchi kuchukua hatua badala ya kuendelea kulalamika kila kukicha
“Wananchi lazima wahakikishe wanazuia na kudhibiti vyombo
vya dola, si muda wa kulalamika tena, wasikubali kuonewa, lazima wachukue
hatua.”
Vilevile Dk Mashinji alisema hatua nyingine inayopaswa
kuchukuliwa ni wananchi wenyewe kumwajibisha mtu atakayekubali kutangazwa
mshindi wakati hastahili
“Wananchi wasikate tamaa, adui namba moja ni aliyetangazwa
mshindi ilihali hakushinda. Ni rahisi sana, hawa watu wanaishi katika jamii
zetu. Kwa mfano sisi Wasukuma watu wanaofanya makosa tunawatenga na kuwapa
adhabu kali za kijamii,” alisema katibu huyo
“Wasihangaike na polisi, wahangaike na wagombea, itafika
mahali hata wakitaka kuwapa ushindi wa hila wataogopa kuukubali.”
Dk Mashinji alisema wananchi wenyewe wanapaswa kujua thamani
ya vyama vingi kuwa kutokubali kuburuzwa
Akizungumzia uchaguzi huo, mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Iringa
(UoI), Jimson Sanga alisema kwa muda mrefu vyama vya upinzani vimeshindwa
kufuata taratibu za kisheria pindi vinapofanyiwa mambo yasiyopaswa na kubaki
kulalamika
“Kama wana malalamiko na kuona wameonewa ni vizuri sasa
wakafuata taratibu kwani chaguzi zinaongozwa na sheria, wafuate utaratibu wa
kwenda katika vyombo vya maamuzi kama mahakama na kuonyesha vielelezo vyote
ambavyo vitawasaidia,” alisisitiza
Hata hiyo, Sanga alisema endapo wapinzani hawana malalamiko
na chaguzi zimefanyika kwa haki, ni wazi kwamba sasa Serikali imeamua kujibu
ajenda zao, hivyo wanapaswa kujipongeza kwa hilo
“Wajitathmini na kuangalia nini hasa kimetokea, kama
wanaamini hawakutendewa haki na wana ushahidi wa hilo waende hata mahakamani
wakadai stahili yao,” alisema
Akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi ndogo za
makao makuu ya CCM jijini Dar es Salaam, katibu mkuu wa chama hicho, Dk Bashiru
Ally alisema wamewapa matumaini wananchi kiasi cha kuaminiwa na hivyo kushinda
uchaguzi huo
“Ninashawishika kusema tumeanza kufanya kazi inayowapa watu
matumaini hasa wanyonge. Kila tulipopita tunazungumza lugha za matumaini na
pengine tukikuta kero tunatatua,” alisema
Dk Bashiru aliongeza kuwa kila walipopita katika mikutano
yao walihimiza mshikamano na kukirudisha chama hicho kwenye misingi ya Azimio
la Arusha pamoja na Mapinduzi ya Zanzibar
Alitaja siri nyingine kuwa ni ya kuwatumia viongozi wastaafu
akiwamo aliyekuwa katibu mkuu wa chama hicho, Yusufu Makamba
“Tumefanya mikutano ya nje na ndani. Mimi nimefanya mikutano
25 ya ndani, nimezungumza na viongozi wa dini 11 na mtu mmoja mmoja,” alisema
Akizungumzia vyama vya upinzani, alisema hawakuwa
wamejipanga badala yake waliishia kupiga porojo kwenye mitandao ya jamii
“Ni wakati muhimu kujiuliza ni aina gani ya siasa
tunazofanya. Tujiulize ni wapi tulipotoka na tunapokwenda. Napenda kuwashukuru
Watanzania kwa imani yao na tutaitumia kuwalipa. Hatutadeka wala kubweteka,”
alisema Dk Bashiru
Aliongeza kuwa, “tunawaahidi utumishi wa uadilifu, tutatumia
rasilimali za nchi kwa manufaa yao.”
Katika Jimbo la Buyungu mgombea wa CCM, Chiza alipata kura
24,578 akifuatiwa na mgombea wa Chadema aliyepata kura 16,910
Msimamizi wa uchaguzi katika jimbo hilo, Lusubilo Mwakabibi
alimtangaza Chiza baada ya kuwashinda wagombea wengine kutoka Demokrasia Makini
aliyepata kura 11; UMD 12; NRA 17; UPDP 18; DP 22; AFP 51 na ACT - Wazalendo
100
Kwa mujibu wa msimamizi huyo ambaye ni mkurugenzi mtendaji
wa Halmashauri ya Kakonko, idadi ya watu waliojiandikisha ni 61,980, lakini
waliopiga kura walikuwa 42,356 huku kura halali zikiwa 41,841 na zilizoharibika
515
Akizungumza mara baada ya kutangazwa mshindi, Chiza alisema
yuko tayari kuwatumikia wananchi wa jimbo hilo na kuwaahidi utumishi uliotukuka
Alisema wananchi wa Buyungu wanakabiliwa na changamoto
mbalimbali ambazo zinahitaji ufumbuzi na akishaapishwa ataanza nazo
“Kazi ya mbunge ni kujua matatizo ya wananchi na kuhakikisha
anayafikisha kwa wale wanaoweza kuyatatua na kurejesha majibu anayoyapata kwa
wapigakura,” alisema mbunge huyo mteule
Kwa upande wa kata, CCM imejihakikishia ushindi katika kata
41 baada ya wagombea wake kupita bila kupingwa. Hata hivyo kwa kata zilizosalia
zote zilikwenda chama hicho baada ya wagombea wake kutangazwa washindi wa
uchaguzi uliofanyika juzi
Imeandikwa na Tausi Mbowe, Elias Msuya, Hapioness Tesha na
Muhingo Mwemezi
Chadema waelezea kilichowanyima ushindi
Reviewed by KUSAGANEWS
on
August 14, 2018
Rating:
No comments:
Post a Comment