Atiwa mbaroni kwa ‘kujiteka’ na kuomba Sh 5milioni kwa ndugu zake


Mkazi wa Pasiansi, Mwanza Prosper Lema, anashikiliwa na polisi kwa mahojiano akidaiwa kujiteka na kutoa taarifa kwa ndugu akiwataka watoe Sh5 milioni kama malipo ya kuachiwa huru

Taarifa ya Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi kwa vyombo vya habari imesema tukio hilo lilitokea Julai 18

“Mtuhumiwa alituma ujumbe mfupi wa maneno kwa njia ya simu kwa ndugu zake akiomba atumiwe Sh5 milioni ili aachiwe na watu aliodai walimteka alipokuwa akitembea kwa miguu katika barabara ya Kenyata katikati ya jiji la Mwanza,” amesema Kamanda Msangi

Amesema baada ya kupokea ujumbe huo, ndugu walitoa taarifa Kituo cha Polisi Kirumba ndipo makachero wa polisi walipoanza kufuatilia mawasiliano ya simu iliyotumika kutuma ujumbe huo na kubaini mtumaji alikuwa eneo la Ngudu wilayani Kwimba wakati akituma ujumbe

“Makachero hao walifanikiwa kumpata mtuhumiwa akiwa amejifungia peke yake moja ya vyumba vya nyumba za kulala wageni akiwa na  simu ya kiganjani iliyotumika kutuma ujumbe akiomba atumiwe fedha,” amesema

Kamanda huyo amesema kitendo cha mtuhumiwa licha ya kuzua taharuki na hofu miongoni mwa ndugu, pia ni kinyume cha sheria

“Kwa hivyo mtuhumiwa atafikishwa mbele ya vyombo vya sheria kwa hatua zaidi mara upelelezi wa awali utakapokamilika,” amesema

Atiwa mbaroni kwa ‘kujiteka’ na kuomba Sh 5milioni kwa ndugu zake Atiwa mbaroni kwa ‘kujiteka’ na kuomba Sh 5milioni kwa ndugu zake Reviewed by KUSAGANEWS on August 02, 2018 Rating: 5

No comments: