Wanafunzi wanne wa kidato cha nne katika Sekondari ya
Kimbiji jijini Dar es Salaam wamefariki dunia baada ya kuzama katika ufukwe wa
Bahari ya Hindi eneo la Kimbiji
Waliofariki wametajwa kuwa ni Queen Madala (16), Selestina
Malipesa (16), Cecilia Ernest (17) na Agneta Philipo (17).
Akizungumza na Mwananchi jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa
Kipolisi wa Temeke, Emmanuel Lukula alisema tukio hilo lilitokea Jumamosi jioni
wakati wanafunzi hao wakiogelea ufukweni baada ya kupelekwa na walimu wao
“Walimu waliamua kuwapeleka wanafunzi hao wa kidato cha nne
ili kuwapongeza wenzao waliofanya vizuri katika mitihani ya mock (majaribio),”
alisema Lukula
“Walikuwa na vyakula na michezo mbalimbali, lakini baadaye
waliingia kuogelea ambapo hao wanne walizidiwa nguvu na maji na mmoja alifariki
hapohapo na wengine hadi kufikishwa Kituo cha Afya Kimbiji daktari
alithibitisha kufariki kwao.”
Alisema walioshuhudia walisema wanafunzi hao walipoanza
kuzidiwa nguvu na maji walikuwa wakitapatapa ndipo wenzao walipiga yowe ya
kuomba msaada
“Wenzao wanaojua kuogelea, wakisaidiana na walimu na watu
waliokuwa katika maeneo hayo walifanya jitihada za kuwatoa majini kabla ya gari
ya wagonjwa kufika na kuwakimbiza kituo cha afya,” alisema Lukula
Alisema Jeshi la Polisi linaendelea kufanya mahojiano na
walimu wao ili kujiridhisha kabla ya kuchukua hatua zinazostahili ikiwemo
kufahamu ni kwa sababu gani waliwapeleka wanafunzi hao ufukweni bila ya kuwa na
tahadhari
“Pasipo kutambua kuwa unapopeleka watoto wengi ufukweni kuna
miongoni mwao wanajua kuogelea na wengine hawajui, ila wao walisahau
kuliangalia hilo na kuruhusu wanafunzi wote kuingia kwenye maji.”
Wanafunzi wanne wafa Maji Dar
Reviewed by KUSAGANEWS
on
July 31, 2018
Rating:
Reviewed by KUSAGANEWS
on
July 31, 2018
Rating:


No comments:
Post a Comment