Mwigulu, Nape na Ummy Mwalimu waungana kwa hili


Kufuatia kifo cha Mbunge wa Korogwe vijijini (CCM), Stephen Ngonyani maarufu kama Prof. Maji Marefu kilichotokea usiku wa kuamkia leo kimeweza kumuibua aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Dkt. Mwigulu Nchemba na kuunga na viongozi wengine wa CCM katika kutoa salamu za pole.

Dkt. Mwigulu ambaye amevuliwa nyadhfa zake na Rais Magufuli mwishoni mwa wiki iliyoisha kupitia mtandao wake wa kijamii amesema kwamba CCM imepata pigo kubwa kwa kumpoteza kada na kiongozi wa kweli.

"Maandiko matakatifu yanasema, mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke siku zake za kuishi si nyingi. Tumempoteza kaka, ndugu na rafiki comrade Stephen Hilary Ngonyani(Prof. Maji Marefu), tumempoteza kiongozi na kada kweli kweli wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)", ameandika Mwigulu.

Mbali na Mwigulu, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu ametoa pole zake kwa familia huku akiwataka wawe na ustamilivu katika kipindi hiki kigumu walichokuwa nacho.

"Mbele yako, nyuma yetu. Pumzika kwa amani kaka yetu Stephen Ngonyani (Prof. Maji Marefu). Natoa pole nyingi kwa familia, ndugu, jamaa na wananchi wa Korogwe Vijijiji. Mwenyezi Mungu awape ustamilivu katika kipindi hiki kigumu", ameandika Ummy.

Pamoja na hao pia Mbunge wa Jimbo la Mtama, Nape Nnauye ameguswa na kifo hicho cha kada mwenzao wa CCM na kumuombe dua marehemu huko aendapo.

"Kaka na rafiki wa kweli, pumzika kaka", ameandika Nape.

Mbunge huyo wa Korogwe vijijini, Steven Ngonyani amefariki akiwa katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili Jijini Dar es Salaam alipokuwa akipatiwa matibabu ya maradhi ambayo yaliyokuwa yanamsibu na kufanya idadi ya Wabunge waliofariki kufikia watano hadi hivi sasa wakiwemo wanne wa majimbo na mmoja wa viti maalumu.


Mwigulu, Nape na Ummy Mwalimu waungana kwa hili Mwigulu, Nape na Ummy Mwalimu waungana kwa hili   Reviewed by KUSAGANEWS on July 03, 2018 Rating: 5

No comments: