Kushuka ghafla kwa mapato yatokanayo na madini ya Tanzanite
kutoka Sh444 milioni hadi Sh40 milioni kwa mwezi kumeanza kuwaathiri wakati wa
Arusha na Mirerani kutokana na kupungua kwa mzunguko wa fedha, Mwananchi
linaripoti
Wiki iliyopita mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris
Kikula na wajumbe wake walitembelea mgodi wa Mirerani na kuwaambia waandishi wa
habari kuwa wamebaini utoroshaji wa Tanzanite uliosababisha kushuka mrabaha
kutoka Sh444 milioni hadi Sh40 milioni kwa mwezi
Alisema wamebaini kuwapo udanganyifu unaofanywa na madalali
wanaonunua madini migodini. “Madalali hawa wakitoka kununua madini wamekuwa
wakipita getini, baadhi wanahofiwa kuficha madini hasa kutokana na kukosekana
vifaa vya kisasa vya upekuzi,” alisema Profesa Kikula
Licha ya ujenzi wa ukuta kuzunguka migodi ya Tanzanite,
Profesa Kikula alisema pamoja na sababu nyingine wanaamini kuna utoroshwaji wa
madini hayo
Maisha ya wananchi Uchunguzi wa Mwananchi katika mji wa
Arusha na Mirerani umebaini kuwa biashara kadhaa zimeanza kukosa wateja huku
hali hiyo ikijidhihirisha wazi katika maisha ya wakazi wa maeneo ambayo
wachimbaji wamekuwa wakikutana
Hali katika baadhi ya klabu za starehe, hoteli na maeneo ya
kuuza madini imeanza kubadilika kutokana na kupungua kwa wateja
Uchunguzi huo umebani kupungua kwa kiasi kikubwa cha wateja
katika klabu maarufu ambazo siku za nyuma zilikuwa ‘zikijaza’ wateja hata siku
za mwishoni mwa wiki
Jeremiah Mollel, mfanyabiashara mjini Arusha anasema
kudhibitiwa kwa biashara ya madini kumechangia kupungua wateja
Katika eneo la jengo la OTTU na maeneo ya St Thomas, ambapo
kawaida huwa na idadi kubwa ya wauzaji wa madini, pia watu wamepungua sana
kutokana na kukosekana kwa madini
Dalali wa madini, Raphael Wandiba anasema baada ya biashara
ya Tanzanite kuwa ngumu, madalali wengi wamehamia migodi ya Ruby wilayani
Longido
“Hapa biashara ni ngumu sana, hakuna madini ya Tanzanite
ambayo yanafika mjini,”alisema
Hali ya maisha katika maeneo kadhaa ya mji wa Mererani
imeanza kuwa ngumu kwa kile wakazi wanachoeleza kuwa ni kutokana na kudhibitiwa
madalali wa madini na wafanyabiashara wengine kuingia migodini
Peter Kaaya anasema tofauti na siku za nyuma, sasa mzunguko
wa fedha katika mji huo umepungua sana. “Mtu kukupa hata Sh5,000 imekuwa ni
ngumu. Zamani ukiomba mtu atakupa hata Sh50,000 lakini sasa kila mtu ana hali
ngumu, nadhani udhibiti wa biashara ya madini umechangia,”alisema
Mwenyekiti wa Chama cha Wauzaji wa Madini Tanzania (Tamida),
Sammy Mollel anaamini kuwa mapato ya Serikali yameshuka na hali ya maisha
imekuwa ngumu kutokana na uzalishaji wa madini kupungua
Anasema Tamida ilipokea kwa mshtuko mkubwa taarifa ya Tume
ya Madini kuwa kushuka kwa mapato kumetokana na utoroshwaji wa madini. “Sisi
tunachojua ni kwamba uchimbaji umedorora na hata kama bado kuna watoroshaji
usingesababisha pengo kubwa la mrahaba
“Hata kama kungekuwepo utoroshwaji wa madini hayo,
haiwezekani kwa mwezi kusababisha hasara ya milioni 400, sisi tunaamini
uzalishaji madini umeshuka na migodi mingi imesimama,” anasema
Anasema hali hiyo haiathiri Serikali tu, bali hata
wachimbaji na wananchi kwani kuna zaidi ya watu milioni moja katika jiji la
Arusha na Mirerani wanaotegemea biasara ya Tanzanite
“Serikali inachopaswa kufanya sasa ni kuwasaidia wachimbaji
wadogo kupata wataalamu na teknolojia za kisasa za kuchimba madini lakini pia
mabenki yaanze kutoa mikopo kwa wachimbaji wa madini,”anasema
Anasema Serikali inapaswa kufanya tafiti za kina katika
migodi ili kujua maeneo yenye madini na kujua yapo umbali gani ili kurahisisha
uchimbaji jambo ambalo litafanya Serikali kupata mapato
Anasema sababu ya pili ya kushuka mrahaba wa Serikali ni
kuwa zaidi ya migodi 10 iliyokuwa inachimbwa katika eneo la Kitalu B na D
ambalo lipo mpakani na kitalu C kinachomilikiwa na Tanzanite One imesimamisha
uzalishaji
“Uchimbaji umesimama kutokana na makubaliano ambayo
yalifikiwa na pande zote kufanya uchimbaji kwa kushirikiana hasa katika maeneo
ya mgogoro na sasa kutokana na Tanzanite One kusimamisha uchimbaji imekuwa
ngumu hata migodi mingine kufanya kazi,”anasema
Mmoja wa wakurugenzi wa Tanzanite One, Faisal Shabhai
anakiri kuwa shughuli za uchimbaji Tanzanite One zimesimama na kwamba zitaanza
siku chache zijazo.</p></div><div><p>Katibu wa
wachimbaji Mirerani, Abubakar Madiwa anasema hali ya maisha kwa wakazi wa
Mirerani wanaotegemea madini ni ngumu, kwani biashara nyingi zimesimama na
hakuna mzunguko wa fedha
“Hapa kuna akinamama ambao huingia migodini kuuza vyakula,
kuna wafanyabiashara wa maji, kuna madalali wa vichenga vya madini, sasa ghafla
kuwazuia hawa wote kuingia ni tatizo,” anasema
Anasema wao hawawaungi mkono wanaotaka kutorosha madini bali
wanachotaka ni kuona Serikali inakusanya mapato yake na wananchi wananufaika
moja kwa moja na madini yao
Wachimbaji wengine wanaamini kuwa kushuka kwa mrabaha pia
kumechangiwa na baadhi ya wamiliki wa migodi na madalali kubaini mbinu mpya ya
kukwepa kuilipa Serikali na kutoroshwa madini
Wamiliki migodi wazungumzia
Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji wa Madini Mkoa wa Manyara
(Marema), Sadick Mnenei anasema kwa ujumla uchimbaji na biashara ya Tanzanite
vimedorora
Anasema taarifa ya hivi karibuni ya Tume ya Madini imefanya
uchimbaji wa madini kuwa mgumu zaidi kutokana na kuongezeka kwa udhibiti wa
vyombo vya usalama katika kuingia mgodini.</
“Sisi tunaamini kushuka kwa mapato ya Serikali hapa Mererani
hakusababishwi kwa kiasi kikubwa na utoroshwaji madini bali kushuka kwa uzalishaji
wa madini
“Sisi wamiliki wa migodi tunajua tunapoanza kupata madini
biashara ya kuuza madini na maisha ya Mirerani hadi Arusha hubadilika na kuwa
bora na mrabaha wa Serikali utaongezeka,” anasema
Anasisitiza kuwa madini ya Tanzanite hayawezi kutolewa kwa
kificho. “Kama mgodi unatoa madini kila mtu atajua kwani kuna wachimbaji wadogo
zaidi ya 50 kila mgodi… kuna wasimamizi na maofisa madini,”anasema
Anasema Marema inaunga mkono jitihada za Serikali katika
kuhakikisha madini ya Tanzanite yananufaisha Watanzania wote na hivyo kuzuiwa
njia yoyote ya kutoroshwa madini nje ya nchi
Maisha ya Arusha na kilio cha kudorora Tanzanite
Reviewed by KUSAGANEWS
on
July 30, 2018
Rating:
Reviewed by KUSAGANEWS
on
July 30, 2018
Rating:


No comments:
Post a Comment