Mfululizo wa ajali za barabarani mkoani Mbeya umemshusha
cheo mkuu wa Usalama Barabarani mkoani humo, Leopold Fungu
Uamuzi wa Fungu kushushwa cheo ulitolewa jana na waziri mpya
wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola jijini Dar es Salaam ikiwa ni saa chache baada
ya ajali nyingine iliyoua watu watano
Lugola alimuagiza katibu mkuu wa wizara hiyo, Meja Jenerali
Jacob Kingu kumshusha cheo Fungu ambaye alikuwa mrakibu wa polisi hadi kubaki
na nyota tatu ikiwa na maana anakuwa mrakibu msaidizi wa polisi
Pamoja na uamuzi huo, Lugola pia aliagiza kushushwa cheo kwa
kamanda wa Kikosi cha Zimamoto mkoani Kagera, George Mrutu
Hata hivyo, alisema alipanga kuwafukuza kazi Mrutu na Fungu,
lakini hakufanya hivyo kwa kuwa jana ilikuwa siku yake ya kuzaliwa
“Niliamua kuagiza wafukuzwe kazi, lakini kwa bahati mbaya na
nzuri kwao mimi nilizaliwa siku ya Ijumaa na leo ni siku ya Ijumaa,” alisema
Lugola
“Siku ambayo nimezaliwa kuna kitu kinaitwa happy birthday
(heri ya kuzaliwa). Sasa wakati naimbiwa happy birthday napaswa kufurahi
kufurahi.Halafu huku unasema fukuzeni hao basi hata hako kafuraha sitokapata
kwa uhalisia, hii ndio bahati kwao.”
Alisema pengine angefanya hivyo siku tofauti, askari hao
watakiona cha moto kwa kuwa sheria ziko wazi, hivyo ametuma salamu kwa Polisi
na Zimamoto kuwasimamia vizuri askari na kuwabadilisha kimtazamo
“Nyakati hizi siyo zile za mwaka ‘47, Serikali ya John
Magufuli inataka vyombo vyake kuwa kielelezo na kioo,” alisema
Lugola aliyekuwa katika kikao cha kimkakati cha viongozi wa
taasisi za wizara hiyo pia alimfukuza kikaoni kamishna mkuu wa Magereza, Dk
Juma Malewa kwa kuchelewa kikaoni
Waziri huyo aliagiza mlango wa chumba walimokuwa wakifanyia
kikao ufungwe itakapotimu saa 5:00 asubuhi na Dk Malewa aliingia kikaoni saa
5:01 na akaamriwa kuondoka
Licha ya kuomba msamaha, Lugola alikataa kumruhusu kuingia
kikaoni.
Wakati Lugola akiagiza Fungu ashushwe cheo, usiku wa kuamkia
jana kulitokea ajali iliyosababisha vifo vya watu watano na mmoja kujeruhiwa
eneo la mlima wa Igawilo iliyohusisha gari dogo aina ya Noah na lori
Katika ajali hiyo, lori lililokuwa na mizigo lilifeli breki
likiwa mlimani na kuigonga Noah, kisha kuilalia.
Fungu aliyekuwepo
eneo la tukio hadi wakati taarifa za kushushwa kwake cheo zinatolewa na Waziri
Lugola, alisema shughuli za uokoaji zilikuwa ngumu kutokana na lori hilo kuwa
na mizigo mingi mizito
Ajali ya jana ni mfululizo wa ajali zilizotokea mkoani humo
ambapo Julai 2, lori liliangukia mabasi madogo matatu na kusababisha vifo vya
watu 20
Juni 14 watu 13 walifariki dunia, wakiwamo vijana 11
waliokuwa mafunzoni wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), katika ajali iliyotokea
kwenye mteremko wa Igodima
Julai Mosi, Rais John Magufuli alifanya mabadiliko madogo ya
baraza la mawaziri na kumuondoa Mwigulu Nchemba katika uwaziri wa Mambo ya
Ndani na Lugola kuteuliwa kushika nafasi hiyo
Kadhalika, Rais aliagiza kuchukuliwa hatua kwa makamanda wa
polisi wanaosuasua katika utekelezaji wa majukumu yao ikiwamo kukabiliana na
matukio ya ajali za barabarani
“Nimechoka kutuma salamu za rambirambi, kila siku inatoka
ajali hii, inakuja hii. Kwa bahati mbaya ni mimi ninayetuma rambirambi, waziri
wa Mambo ya Ndani hahangaiki...” alisema Rais wakati akimwaapisha Lugola na
viongozi wengine aliowateua hivi karibuni
Ajali Mbeya zamshusha cheo kigogo wa polisi akiwa eneo la ajali
Reviewed by KUSAGANEWS
on
July 07, 2018
Rating:
Reviewed by KUSAGANEWS
on
July 07, 2018
Rating:


No comments:
Post a Comment