Mtandao wa wanafunzi wageuka mbogo masharti ya mikopo elimu ya juu


Mtandao wa Wanafunzi Tanzania(TSN) wameiomba  Bodi ya Mikopo ya Elimu  ya  Juu (HESLB) kushughulikia baadhi ya vipengele vinavyozungumzia sifa za mwanafunzi anayepaswa kupata mikopo, kwa maelezo ni kandamizi na vinawanyima fursa wanafunzi .

Moja ya kipengele hicho  ni kile cha mwanafunzi  ambaye ana mzazi au mlezi ayemiliki biashara au kampuni inayotambulika na mamlaka za usajili, kutoruhusiwa kuomba mkopo

Akizungumza leo Mkuu wa Idara ya Haki ya Wanafunzi wa mtandao huo, Gibson Eliaform amesema, “Meneja ni cheo tu hakitambulishi uwezo wa mtu hata mwenye kibanda cha huduma za fedha kwa mitandao ya simu na kampuni ndogo iliyosajiliwa anaweza kuwa meneja wa biashara.”

“Anaweza kuwa amesajili biashara yake Brela (Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni ) au TRA (Mamlaka ya Mapato Tanzania) na ana mtaji wa Sh500,000 je huyu ni tajiri?” amehoji.

 Amesema kipengele kingine ni kinachozuia wanafunzi waliotajwa katika sheria ya utumishi wa umma kutoomba mikopo, ikiwamo madiwani, maofisa watendaji wa kata na mtaa ambapo kimsingi kazi yao haina mshahara.

 Eliaform amesema kigezo hicho hakipo kisheria na huenda kimewekwa makusudi ili kupunguza wanufaika wa mikopo kulingana na bajeti

Amesema kipengele kingine kinachotakiwa kufanyia marekebisho ni kuzuiwa wanafunzi waliosoma shule binafsi, kubainisha kusoma shule binafsi siyo kigezo kinachotambulisha uwezo wa mzazi kuhimili gharama za masomo Chuo Kikuu

 “Hali hubadilika kuna kufilisika, magonjwa na pia wanaolipa ada ndogo chini ya Sh1 milioni kuwanyima mikopo ni kukatisha ndoto zao,” amesema.
Mtandao wa wanafunzi wageuka mbogo masharti ya mikopo elimu ya juu Mtandao wa wanafunzi wageuka mbogo masharti ya mikopo elimu ya juu Reviewed by KUSAGANEWS on May 22, 2018 Rating: 5

No comments: