Wilaya hatari kwa malaria zatajwa


Watu 720,181 wameripotiwa kuugua ugonjwa wa malaria katika vituo mbalimbali vya afya kwa miaka mitatu iliyopita mkoani Pwani
Idadi hiyo ni takriban asilimia 15 zaidi ya kiwango cha maambukizo ya kitaifa, ambayo ni asilimia 14

Takwimu za idara ya afya mkoani Pwani, zinabainisha wilaya na kiwango cha maambukizi yake kwenye mabano ni Halmashauri ya Chalinze (131,197); Mkuranga (127,740); Kibiti (114,584); Kisarawe (90,079); Rufiji (80,910); Kibaha vijijini (60,286); Mafia (53,461); Kibaha mjini (36,963); na Bagamoyo (24,958).

Kwa mujibu wa Ofisi ya Takwimu ya Taifa (NBS), Mkuranga inakadiriwa kuwa na watu 243,062 kwa maana hiyo nusu yao waliugua ugonjwa huo; Kisarawe yenye watu 110,777 takriban asilimia 87 walipata malaria; na Kibiti yenye 133,727 wote waliugua malaria

Takwimu hizo zilimshtua mkuu wa Mkoa wa Pwani, Evarist Ndikilo na kulazimika kuandaa kampeni maalumu ya uhamasishaji matumizi ya dawa za kuulia viluwiluwi vya mbu, ambayo aliizindua jana katika viwanja vya Mailimoja na kuhudhuriwa na wadau wa afya.

Ndikilo alisema mwaka 2016 wagonjwa walioripotiwa ni 211,810 na mwaka 2017 waliongezeka hadi 268,394 na kwamba, anashindwa kujua kiini cha tatizo hilo ilhali kiwanda cha dawa za mbu kipo mkoani hapa. Pwani inakadiriwa kuwa na idadi ya watu 1,197,933
“Dawa za kuulia viluwiluwi vya mbu zinatengenezwa hapa Kibaha napata shida kuelewa sababu za idadi kuwa hivi, ukiangalia Rais (John Magufuli) alishaagiza halmashauri zinunue kwa ajili ya watu wao, nikiuliza naambiwa wananunua,” alisema Ndikilo na kuhoji:

“Je, tatizo lipo wapi wanafungia stoo? Sasa nafuatilia hili jambo kwa umakini zaidi.”

Ndikilo alibainisha kuwa amedhamiria kuongeza matumizi ya viuatilifu hivyo ili kudhibiti mbu na kwamba, siku ya kwanza ya kampeni ya uhamasishaji matumizi ya dawa hizo watatoa bure dawa za thamani ya Sh1,056,000 kwa baadhi ya wananchi na watatoa elimu kwa vitendo

Pia, aliagiza wakurugenzi wote kuhakikisha wananunua dawa hizo na kuwafikishia wananchi siyo kuziweka stoo na kwamba, ili kuhakikisha utekelezaji unafanyika kama alivyoagiza Rais Magufuli mwaka jana atatumia vyombo vyake mbalimbali

“Mkurugenzi atakayekwenda kinyume na agizo hili atakuwa amekwenda kinyume na agizo la rais. sheria ipo wazi mtumishi yeyote anayekwenda kinyume na maagizo ya rais ina maana hatoshi atabidi atupishe tu, hatutaki hizi takwimu tena,” alisema

Awali, mganga mkuu Mkoa wa Pwani, Dk Yudas Ndungile alisema mwaka jana malaria ilikuwa ugonjwa wa pili kati ya magonjwa makuu matano yanayoogoza kwa vifo na iliua watu 57

Naye mkazi wa Mailimoja Kibaha, Gustaph Elius alipongeza hatua ya mkuu wa mkoa kwa kuanzisha kampeni ya malaria inawakutanisha wananchi wa ngazi zote pamoja na kuelimishwa matumizi sahihi ya dawa za viuatilifu vya malaria, kwa kuwa bila elimu hata wakipewa bure inaweza ikawa kazi bure.
Wilaya hatari kwa malaria zatajwa Wilaya hatari kwa malaria zatajwa Reviewed by KUSAGANEWS on April 14, 2018 Rating: 5

No comments: