SERIKALI YA KENYA YAWEKA MIKAKATI KUIMARISHA SEKTA YA ELIMU YA KIUFUNDI


NAIBU Rais William Ruto amesema serikali imeanzisha mpango wa kuifanya elimu ya kiufundi (Technical Vocational Education and Training-TVET) kuwa ya kuvutia kote nchini.

Alisema elimu ya kiufundi sio ya wale waliogura shule lakini ni ya wanafunzi waliokirimiwa talanta ambazo zinaweza kuwawezesha kufaulu maishani.

Akiongea afisini mwake, jumba la Harambee Annex, alipokutana na maafia wakuu wa Wizara ya Elimu na Fedha, Naibu Rais alisema mikakati imewekwa kuondoa dhana kuwa mafunzo ya kiufundi yametengewa wanafunzi ambao hawakupata alama za juu mitihani ya kitaifa.

"Tunafanya kila tuwezalo kutoa nafasi kwa wanafunzi kupata elimu bora. Tunafanya hivi kwa kuboresha vyuo vya kutoa mafunzo hayo ili vifikie viwango vya kimataifa.

Tumetenga fedha za kununua vifaa vya kisasa vya mafunzo ili wanafunzi waweze kupata ujuzi mwafaka wanapohitimu," akasema Bw Ruto bila kufafanua zaidi.

Bw Ruto alisema elimu ya kiufundi inaweza kuimarisha uchumi wa nchini kwa kutoa nafasi kuimarisha ujuzi wao ili wapate ajira katika sekta za kiufundi kama viwandani.

"Waliohitimu kwa mafunzo ya kiufundi wanaweza kusaidia kustawisha sekta ya utengenezaji bidhaa, ambayo ni mojawapo ya ajenda nne za maendeleo ya serikali ya Jubilee. Tunapaswa kuwa na nguvu kazi ya kutosha yenye ujuzi ili kutosheleza mahitaji ya kiteknolojia katika taifa leo," Naibu Rais akasema.

Mipango kukamilika

Ruto alisema Wizara ya Elimu imekamilisha mipango ya kuhakikisha kuwa wanafunzi wanaosomea masomo ya kiufundi wanapata mikopo kutoka kwa serikali.

"Ama kwa hakika wanafunzi 27,000 kutoka vyuo mbalimbal vya kiufundi sasa wanapaswa kupata mikopo hiyo," akaongeza, kauli yake ikithibitishwa na Katibu katika Wizara ya Elimu Belio Kipsang'.

Mkutano huo pia ulihudhuriwa na Mawaziri wa Elimu Amina Mohammed na mwenzake wa Fedha Henry Rotich.

SERIKALI YA KENYA YAWEKA MIKAKATI KUIMARISHA SEKTA YA ELIMU YA KIUFUNDI SERIKALI YA KENYA YAWEKA MIKAKATI KUIMARISHA SEKTA YA ELIMU YA KIUFUNDI  Reviewed by KUSAGANEWS on April 05, 2018 Rating: 5

No comments: