Mbunge wa Viti Maalumu (Chadema), Cesilia
Pareso amesema ukiacha maadui watatu wa Taifa ambao ni maradhi, umasikini na
ujinga ameongezeka adui namba nne ambaye ni vyama vya siasa vya upinzani.
Akizungumza leo Alhamisi Aprili 5, 2018
katika mjadala wa bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu mwaka 2018/19 bungeni mjini
Dodoma, Pareso amesema vyama vya upinzani ni adui mwingine kwa kuwa kwa sasa
vinapigwa vita na Serikali iliyopo madarakani, ikiwa ni pamoja na kuzuiwa
kufanya shughuli za siasa
Mbunge huyo pia amegusia chaguzi ndogo
zilizofanyika hivi karibuni, kubainisha kuwa zilikuwa ni kati ya Chadema na
Jeshi la Polisi sambamba na kueleza jinsi wabunge na madiwani walivyonunuliwa
na kuvihama vyama vyao, nchi kulazimika kufanyika chaguzi nyingine alizodai
aimegharimu zaidi ya Sh6 bilioni
Maelezo ya Pareso yalipingwa na baadhi ya
wabunge na wengine kumuunga mkono huku Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu
Nchemba akimjibu mbunge huyo kuwahusisha polisi na chaguzi mbalimbali
“Utaendeleaje kupima chama cha siasa kinakua
kama hakifanyi mikutano ya hadhara na kuongeza wanachama, leo mtu anajiunga
kesho mtu anatoka,” amesema Pareso
“Kama mnakataza vyama vya siasa visifanye
mikutano ya hadhara, hamuwezi kuja bungeni na kutueleza vyama hivi vimeendelea
kufanya vizuri miaka 26 iliyopita.”
Huku akizungumza kwa upole Pareso amesema,
“Miaka ya nyuma waasisi wa nchi hii waliwaaminisha Watanzania kwamba kuna
maadui watatu ambao ni umaskini, ujinga na maradhi lakini kwa
yanayoendelea leo, jambo jingine limeongezeka kwa Serikali iliyopo madarakani.
Adui mwingine ni vyama vya siasa.”
Amesema siku za hivi karibuni wabunge na
madiwani wa vyama vya siasa, hasa upinzani wamekuwa wakiripoti polisi na
kuwekwa rumande, hata kama wataachiwa wataendelea kuripoti polisi
“Mmeongeza adui mwingine ambaye ni vayama
vya siasa vya upinzani. Tumeshuhudia kwenye changuzi ndogo za marudio, utumiaji
mbovu wa fedha za wananchi. Kama tulitenga fedha za dharura Sh4bilioni endapo
utatokea uchaguzi leo tumetumia Sh6.9bilioni,” amesema
“Kwanini tusingefikiria kuhifadhi hizi
hela kuliko kurudisha wananchi kufanya chaguzi tena kwa sababu tu watu
wameamua kununua watu warudi upande wa pili.”
Amesema chaguzi hizo za marudio zilikumbwa
na ukiukwaji wa taratibu za uchaguzi, “tumeshuhudia uchaguzi kati ya Chadema na
Jeshi la Polisi. Nilishuhudia wakala anatekwa kituoni polisi yupo na hasemi
kitu.”
“Ushauri wangu kwa Waziri Mkuu (Kassim
Majaliwa) kwa sababu inaonekana mmeongeza adui mwingine ambaye hamtaki
kumsikia, ushauri wangu ni kuleta marekebisho ya katiba hapa bungeni. Tufute
vyama vingi ili ulimwengu na dunia ijue kwamba Serikali haitaki
vyama vingi turudi kwenye mfumo wa chama kimoja. Hiyo ni njia
sahihi na mtaendelea kuyafanya mnayoyafanya kama mnavyotaka.”
Wakati Pareso akiendelea kuchangia, Mwigulu
alisimama na kutoa ufafanuzi wa alichokisema mbunge huyo
“Pamoja na kuheshimu uhuru wa kuongea na
kulinda uhuru wa mbunge kutoa maoni yake, nilitaka kuwashauri wabunge
tunapoongelea taasisi ambazo zipo kikatiba na kufanya kazi kwa ajili ya
wananchi tuheshimu kazi zinazofanywa,” amesema Mwigulu
“Hakuna uchaguzi kwa uzoefu wangu ambao
utafanyika bila usalama kuimarishwa. Uhalifu wowote unaofanyika ndani ya nchi,
iwe wakati wa uchaguzi au wakati ambao si wa uchaguzi, unahitaji
kuwahakikishia wananchi usalama kama kawaida.”
Mwigulu amesema uzoefu umeonesha kuwa
muongeaji (Pareso) chama chake kinaposhiriki katika uchaguzi kunakuwa na
matukio makubwa ya uhalifu
“Kuna uchaguzi mmoja chama chako (Chadema)
hakikushiriki hakukuwapo na matukio ya aina yoyote ya utekaji wala maumivu ya
wananchi. Sisi kama Jeshi la Polisi tupo kwa ajili ya kuwahakikishia wananchi
usalama na hatuwezi kuacha wananchi wakakatana mapanga,” amesema.
Baada ya maelezo hayo Pareso aliendelea
kuchangia, “Naomba kumwambia Mwigulu kwa sababu unaingia katika baraza la
mawaziri, pokea ushauri wangu na umueleze Rais Magufuli tufute vyama vya
upinzani nchini.”
Mbunge Chadema aliamsha Dude bungeni kuhusu upinzani
Reviewed by KUSAGANEWS
on
April 05, 2018
Rating:
No comments:
Post a Comment