Maswali 10 kampeni ya Makonda wanawake waliotelekezwa


Wakati Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ikiendelea kusikiliza mashauri ya wanawake na wanaume kuhusu kutelekeza watoto, kampeni hiyo imeibua maswali kadhaa, huku baadhi ya watu wakitaka tahadhari ichukuliwe kuepusha athari

Kwa siku tatu mfululizo sasa, wakazi wa jijini Dar es Salaam, hasa wanawake, wamekuwa wakifurika ofisi hiyo kuwasilisha madai ya kutelekezwa na wazazi wenzao, ikiwa ni kuitikia wito wa Mkuu wa Mkoa, Paul Makonda ambaye ameeleza kuwa anataka kuwasaidia kutafuta suluhisho

Kampeni hiyo imekumbwa na matukio kadhaa, kama ya wanaume kujitokeza wakidai kukimbiwa, wasichana wa umri mkubwa kudai pia wametelekezwa na baba zao, huku Makonda akidai miongoni mwa waliotajwa ni wabunge na viongozi wa dini

Katika nchi ambayo ina utamaduni wa kushughulikia masuala ya ndoa kwa faragha, ina sheria na taasisi za kushughulikia masuala hayo nyeti, kampeni hiyo imeibua hisia tofauti; baadhi wakisifu, wengine wakikosoa, kushauri jinsi ya kutelekeza mradi huo na wengine kuibua maswali kuhusu ufanisi na athari za kitendo hicho

Baadhi ya wasomaji wa Mwananchi wamekuwa wakipiga simu kuulizia uhalali wa kampeni hiyo, huku watumiaji wa mitandao ya kijamii wakiibua hoja za kisheria, kijamii na kiutamaduni kuhusu utekelezaji wa mradi huo

Mwananchi imechambua maswali na hoja hizo na kuziweka katika vipengele kumi na baadaye kuhoji wadau na pia kuchukua maoni ya watu waliojitokeza hadharani, kama bungeni na kwenye akaunti za mitandao ya kijamii, kuzungumzia suala hilo

Maswali hayo yanajikita katika mila na utamaduni wa Kitanzania, sheria kama ya mtoto na ndoa, uwezekano wa mpango huo kutoa suluhisho, utayari wa watuhumiwa kuitikia wito, athari dhidi ya watoto, hadhi ya wahusika na mgongano unaoweza kutokea baina ya taasisi zilizopewa dhamana ya kushughulikia masuala hayo

“Ushauri wangu kama wizara inayosimamia haki za watoto, suala hili linapaswa kufanyika kwa faragha kwa sababu una-deal na watu,” alisema Naibu Waziri wa Afya, Dk Faustin Ndugulile, ambaye wizara yake pia inaongoza Idara ya Ustawi wa Jamii

“Anachokifanya RC Makonda ni jambo zuri, lakini linahitaji uangalifu na tufuate mifumo sahihi. Nitoe wito kwa wananchi wote kufuata taasisi zinazohusika.”

Dk Ndugulile ni mmoja wa watu waliozungumzia suala hilo, wakijibu moja ya maswali yaliyoibuka kuhusu utaratibu wa kushughulikia masuala ya malezi na ndoa, ambayo hushughulikiwa na taasisi zinazohusika kwa njia ya faragha

Kauli yake inatokana na hali iliyojitokeza kwenye ofisi hiyo, ambako wanawake wengi walienda wakiwa wamebeba watoto na kuachia baadhi ya watu kuwapiga picha na baadaye kuzisambaza mitandaoni, ikiwemo picha ya mtoto chotara wa Kichina na Kitanzania, iliyosababisha mama yake kulalamika

Mila na desturi zinasemaje?

Moja ya maswali hayo ni kama kazi hiyo inafuata mila na desturi za Kitanzania

“Kinachofanyika katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa kinakwenda kinyume na mila na desturi za Mtanzania kwa sababu masuala yanayohusu mzozo wa kifamilia na ndoa hufuata ngazi maalumu,” alisema Mwanaharakati wa haki za binadamu na masuala ya jinsia, Gemma Akilimali

“Mara zote kunapotokea mvutano unahusisha wanandoa kutoelewana au utata kuhusu mimba, watu wa kwanza wanaopaswa kutatua tatizo hilo ni familia na inapoonekana suala hilo linashindikana, jamii ya eneo hilo.”<

Kisheria ni sahihi?
Pia suala jingine ni kuhusu sheria

Alipoulizwa kuhusu suala hilo, mkurugenzi wa Chama cha Wanawake Wanasheria Tanzania (TAWLA), Tike Mwambikile alisema kitendo cha wanawake na watoto kupigwa picha na kuonyeshwa kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii si sawa

Hoja kama hiyo ilitolewa na Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu aliyesema tatizo la kampeni hiyo ni kutokuwa na faragha ya watoto licha ya kinachofanyika kuwa ndani ya sheria huku wahudumu wakitokea idara ya Ustawi wa Jamii

Alisema ni kosa kisheria kwa chombo cha habari au mitandao ya jamii kuonyesha picha zenye kumdhalilisha mtoto

Kuna mgongano wa kitaasisi?

Kuhusu baadhi ya mashauri kuwahi kuwasilishwa kwenye vyombo husika na hivyo kuwepo uwezekano wa maamuzi kugongana, Akilimali alisema si jambo la busara mkuu wa mkoa kuwakusanya watu sehemu moja na kuanza kusikiliza shida zao na iwapo ataendelea kufanya hivyo atakuwa amezipuuza taasisi nyingine, hivyo kuibua mvutano

Mwantum Mgonja, ambaye ni miongoni mwa wanasheria wanaosikiliza malalamiko hayo, alisema wengi waliofika walianzia ustawi wa jamii na baadhi walifikisha masuala yao mahakamani

Kampeni kutoa suluhisho la kudumu?

Baadhi wanaona jitihada hizo za RC zinaweza zisitoe suluhisho lenye ufanisi na mkurugenzi wa Chama cha Wajane (Tawia), Rose Serwati anaona kampeni hiyo inaweza ikachangia kuvunja ndoa za watu na kuweka uadui kati ya baba, mama na mtoto

Hoja kama hiyo ilitolewa juzi na mbunge wa Ulanga (CCM), Goodluck Mlinga alipotaka ufafanuzi wa kampeni hiyo, akisema njia inayotumika ni ya kubomoa na si kujenga

Lakini mhadhari msaidizi, Taasisi ya Ustawi wa Jamii (ISW), Abigael Kiwelu alimshauri Makonda kutumia fursa hiyo kuelimisha wanawake hao ili wafikishe matatizo yao kwa maofisa ustawi wa jamii walioko kwenye kila kata

Nini kitafanyika kwa wasioitikia wito

Wakati Makonda akitoa kauli kwamba wasioitikia wito kwenda kusikiliza malalamiko dhidi yao watatangazwa, mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo-Bisimba alisema Sheria ya Kanuni za Adhabu sura ya 16 kifungu cha 166 inawataka wazazi kulea na kutunza watoto wao

Alisema mzazi anayekwepa kumlea mtoto au kumtunza hali ana uwezo, wa kumuhudumia atakuwa ametenda kosa la jinai

Alisema Sheria ya Haki ya Mtoto ya mwaka 2009 inawahimiza wazazi na walezi kulea watoto wao na kutimiza majukumu yao yote

Uhakiki wa madai yanayotolewa ukoje?

Katika kinachooneka kutaka uhakika wa madai dhidi ya wabunge wanaotuhumiwa kutelekeza watoto, Spika wa Bunge, Job Ndugai juzi aliwataka wazazi wenye malalamiko hayo waende kwake wakiwa na matokeo ya kipimo cha DNA

Ndugai alisema inabidi ufanyike utaratibu ili kujua namna gani ya kushughulikia suala hilo

Kuna ajenda ya siri?

Hata kabla ya kuanza kusikiliza mashauri hayo, tayari watu kadhaa walishatuhumu kuwa huenda mpango huo una ajenda ya siri na tayari baadhi ya wanasiasa wamesema bayana kuwa kuna njama za kuwachafua

Tuhuma kama hizo ziliibuka pia wakati wa kampeni ya kusaka watumiaji na wauzaji wa dawa za kulevya iliyotaja pia wanasiasa na viongozi wa kidini

Maswali mengine ni pamoja na kama kampeni hiyo itatoa fursa sawa ya kusikilizwa kati ya wanaume na wanawake na kama haki za kibinadamu zitafuatwa

“Unapowaweka watu pale hadharani unavunja haki ya kuwa na faragha. Mtu anaweza kushtaki kama ataona amedhalilishwa,” alisema mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Jesse James

Imeandikwa na Nasra Abdallah, Elias Msuya, Harieth Makwetta, Kalunde Jamal, Raymond Kaminyoge, Tumaini Msowoya, George Njogopa, Sharon Sauwa, Elizabeth Edward na Fortune Francis

Maswali 10 kampeni ya Makonda wanawake waliotelekezwa Maswali 10 kampeni ya Makonda wanawake waliotelekezwa Reviewed by KUSAGANEWS on April 12, 2018 Rating: 5

No comments: