Malema, Zenani wachafua hali ya hewa msiba wa Winnie Mandela

Zenani, mtoto wa mwanamapinduzi wa Afrika Kusini, Nelson Mandela na Julius Malema ambaye ni kiongozi wa chama cha EFF jana, walifanya tukio lisilo la kawaida baada ya kuamua kuwapa vidonge vyao wasaliti na wabaya wa Winnie Mandela mbele ya umati uliofurika kuaga mwili wake kwenye Uwanja wa Orlando

“Mama‚ wale waliokusaliti kwa watawala (enzi za ubaguzi wa rangi) wako hapa,” alisema Malema mbele ya maelfu ya waombolezaji waliofurika kuaga mwili wa Winnie, mke wa rais wa kwanza mweusi wa Afrika Kusini, Nelson Mandela

Zenani pia aliwaliza waombolezaji aliposema mama yake aliporwa haki yake wakati wa maisha yake. Zenani pia alivicharukia vyombo vya habari akisema vilitumika kumchafua mama huyo

“Kwanini waliukalia ukweli na kusubiri hadi mama yangu afe ndipo wauseme? Wamepora urithi wa haki wa mama yangu wakati wa uhai wake,” alisema Zenani huku dada yake Zindzi akiwa pembeni yake

Alionyesha kukasirishwa na kauli ya kamishna wa zamani wa polisi nchini humo, George Fivaz ambaye wiki iliyopita baada ya kifo cha Winnie alisema hakuna kinachomhusisha Winnie na kifo cha Stompie Seipei. Zenani alisema wote waliomfanyia mabaya mama yake wasifikiri hata mara moja familia itayasahau mambo hayo

“Kumsifia sasa hivi kunaonyesha wazi jinsi ulivyo mnafiki,” alisema Zenani akimtaja Fivaz na akaongeza: “Maumivu aliyoyapata maishani mwake yapo kwetu.”

Malema alisema pamoja na huzuni aliyonayo kwa kumpoteza Winnie anafurahia namna alivyofariki dunia, akiongeza kwamba hakuwasaliti watu wake

“Mama wale waliokusaliti kwa watawala wako hapa. Wanalia kwa sauti kubwa kuliko sisi sote tuliokuheshimu‚” alisema katika hotuba yake

Malema aliwataja watu waliomshambulia mama huyo wakati wa uhai wake, kwanza akiwashutumu viongozi wa zamani wa chama cha United Democratic Front (UDF) ambao waliitisha mkutano wa waandishi wa habari wakati wa utawala wa ubaguzi wa rangi ili kutangaza kujitenga na mwanamama huyo



Pia, aliwashambulia viongozi wa ANC ambao walimwita mama huyo kuwa mhalifu na baadaye walimzuia kuzungumza katika msiba wa mwanaharakati kijana, Peter Mokaba
“Wasaliti‚ tunawaona. Maisha hayana usawa‚” alisema Malema.
Aidha kiongozi huyo wa EFF aliwapongeza watu waliosimama kidete na Winnie Madikizela-Mandela wakati alipodhalilishwa
“Winnie Mandela ni mama yetu. Tunamfahamu. Hatumhitaji Fivaz kutuambia chochote kuhusu Winnie Mandela‚” alisema Malema

Alitoa wito kwa wakazi wa Soweto ambako alikuwa akiishi hadi alipofariki dunia, wasimsahau kamwe Winnie Mandela

Pia Malema alipendekeza uwanja wa ndege wa Cape Town upewe jina la Winnie.
Malema, Zenani wachafua hali ya hewa msiba wa Winnie Mandela Malema, Zenani wachafua hali ya hewa msiba wa Winnie Mandela Reviewed by KUSAGANEWS on April 15, 2018 Rating: 5

No comments: