|
Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya
imetumia takriban saa mbili kutoa hukumu iliyowapeleka jela miezi mitano
Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ na Katibu wa Chadema Kanda ya
Nyasa, Emmanuel Masonga.
Hakimu Mkazi Mfawidhi, Michael Mteite
alianza kusoma hukumu saa 3:32 asubuhi hadi saa 5:20 asubuhi jana na kuwatia
hatiani washtakiwa na baadaye kuwahukumu kutumikia adhabu hiyo akisema
amejiridhisha pasipo shaka kwamba walitenda kosa la kutumia lugha ya fedheha
dhidi ya Rais John Magufuli
Washtakiwa walidaiwa kutenda kosa
hilo kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Desemba 30, 2017 katika eneo la
Uwanja wa Shule ya Msingi Mwenge jijini Mbeya.
Hakimu Mteite alisema mahakama
ilijielekeza katika viini (hoja) vikuu kadhaa katika kesi hiyo hadi kufikia
hatua ya kutoa uamuzi.
Kwanza mahakama ilijiuliza maswali
kadhaa katika kesi hii, je ni kweli washtakiwa walitamka maneno hayo? Je
maneno hayo yanabeba maana ya ‘abusive word’ (maneno ya fedheha
“Je, maneno hayo yalimlenga nani?
Na mwisho je maneno hayo yangeweza kuleta hali ya uvunjifu wa amani?
Yalimlenga nani? Lakini pia je, wana hatia au hawana hatia?” alisema Hakimu
Mteite
Maelezo ya hukumu
Hakimu Mteite alianza kwa kutoa
maelezo ya ushahidi uliotolewa na mshtakiwa wa pili (Masonga) kwamba katika
ushahidi wake alijikita zaidi kusema siku ya mkutano hakuhudhuria.
Hakimu Mteite alisema mahakama
haikuona sababu ya kuuchukulia kwa uzito ushahidi huo kwa kuwa aliutoa wakati
upande wa mashtaka ukiwa umemaliza na kufunga ushahidi wake. Alisema Masonga
alipaswa kuuwasilisha awali wakati wa utetezi.
Alisema, “Utetezi wa mshtakiwa wa
pili uliegemea kwamba hakuwepo kwenye mkutano huo, alitoa utetezi kwamba
hakuhudhuria kwa vile alipigiwa simu na mke wake Grace Mallya kuwa anaumwa,
hivyo arudi nyumbani na alipofika hakutoka kwenda popote.”
“Alipaswa kutoa maelezo ya
kutokuwepo eneo hilo awali kabla upande wa mashtaka haujafunga ushahidi wake.
Ikumbukwe kwamba mshtakiwa huyu tangu awali alikuwa na mawakili watano,
lakini mawakili wote hawa hawakuitaarifu mahakama kwamba mshtakiwa wa pili
ataegemea upande fulani katika utetezi wake.
Hivyo mahakama haitaupa uzito
utetezi wa mshtakiwa huyu kwamba hakuwepo eneo la tukio siku hiyo.”
Akijikita katika viini
alivyovitaja awali katika utoaji hukumu hiyo, Hakimu Mteite alisema uhalisia
unaonyesha washtakiwa walitamka maneno hayo kulingana na ushahidi uliotolewa
na mashahidi wa pili, tatu na wa tano
“Mashahidi wa pili, tatu na watano
walikuwa ni wa kuona na kusikia. Hivyo, katika kesi hii hakuna ubishi kwamba
mashahidi hawa walitoa ushahidi wa kuona na kusikia,” alisema.
Alisema mahakama inaamini
washtakiwa walitoa maneno hayo ambayo ni ya fedheha na yalimlenga Rais kwa
kuzingatia baadhi yaliyotamkwa
“Mashahidi walisema maneno yale
yalimlenga Rais John Magufuli. Na hapa ni kweli unapozungumzia masuala ya
kitaifa kama maneno ya kutekwa, kuuawa watu ni masuala ya kitaifa, hivyo
haiwezi kuwa Rais Magufuli mwingine na hata washtakiwa wenyewe walikuwa
wanatamka ‘Rais wetu Magufuli’ hii inatosha kwamba aliyelengwa katika maneno
yale ni Rais Magufuli,” alisema.
Baada ya kueleza hayo, Hakimu
Mteite alisema mahakama imejiridhisha kwamba Sugu na Masonga walitamka maneno
hayo, hivyo inawatia hatiani kwa vile walitenda kosa.
Walichosema mawakili
Hakimu Mteite alitoa nafasi kwa
Wakili wa Serikali Mkuu, Joseph Pande aliyesema upande wa Jamhuri unaridhika
kwamba washtakiwa wote wawili hawana rekodi yoyote ya kutenda makosa, lakini
kwa kuwa wametiwa hatiani aliiomba mahakama kutoa adhabu kali.
“Kwa vile washtakiwa walitoa
maneno ya fedheha dhidi ya Rais wa nchi, tunaomba mahakama itoe adhabu kali
kwa washtakiwa ili iwe funzo kwa wengine pia,” alisema.
Wakili wa utetezi, Peter Kibatala
alisimama na kuieleza mahakama iangalie adhabu ya kuwapatia wateja wake
akibainisha kuwa wamekaa mahabusu kwa takriban mwezi mmoja, hivyo mahakama
ione hiyo ni sehemu ya adhabu japo hawakuwa wafungwa kamili.
Kibatala aliiomba mahakama
kuridhia Sugu na Masonga kupewa adhabu ya kifungo cha nje akisema hilo
litasaidia mambo mengi ikiwamo suala la uvunjifu wa amani unaoweza kutokea
endapo wawili hao watahukumiwa kwenda jela
“Mlengwa katika maneno yale
alikuwa ni Rais Magufuli lakini hiyo haiwezi kumuondolea hadhi yake kwa kuwa
ana uwezo wa kuyajibu maneno yale popote pale. Pia kwa heshima zote kwa Rais,
mwisho wa siku ni mwanasiasa na waliotiwa hatiani kwa kutamka maneno yale ni
wanasiasa ‘so it was a political platfrom’ (ilikuwa ni jukwaa la kisiasa)
hivyo mahakama yako ijielekeze na iyachukulie hivyo hivyo kama ni maneno ya
kisiasa,” alisema.
Kibatala alisema Masonga ni baba
wa familia kama ilivyo kwa Sugu, lakini Sugu pia ni mbunge wa wananchi wa
Mbeya Mjini, hivyo aliiomba mahakama itoe adhabu kulingana na hoja hizo kwa
kuwa katika hilo kuna upande utakaoathirika na si kwa washtakiwa pekee.
Hakimu Mteite baada ya
kuwasikiliza mawakili hao alisema, “Nimezingatia hoja za pande zote mbili,
hivyo washtakiwa watakwenda jela miezi mitano.”
Mwanzo wa kesi
Kwa mara ya kwanza, Sugu na
Masonga walifikishwa mahakamani Januari 16 na kusomewa mashtaka na Wakili wa
Serikali Mkuu, Joseph Pande aliyeeleza upelelezi ulikuwa umekamilika na
walikuwa tayari kuendelea na usikilizaji. Pande zote zilikamilisha ushahidi
Februari 9.
Jamhuri iliwasilisha mashahidi
watano na kielelezo kimoja cha sauti iliyodaiwa kurekodiwa na shahidi wa
tano, Inspekta Joram Magova.
Upande wa utetezi uliwasilisha
mashahidi sita wakiwamo Sugu na Masonga waliokana kutamka maneno
wanayoshtakiwa kuyatoa.
Washtakiwa awali walitetewa na
mawakili Sabina Yongo, Boniface Mwabukusi na Hekima Mwasipu. Mawakili wengine
wa Serikali walioendesha kesi hiyo ni Ofmed Mtenga na Baraka Mgaya.
Upande wa mashtaka ukiongozwa na
wakili Pande uliiomba mahakama kuzuia dhamana kwa washtakiwa akitoa sababu
kwamba ni kwa ajili ya usalama wao ombi lililopingwa na Wakili Yongo akisema
dhamana ni haki ya kikatiba ya washtakiwa.
Hata hivyo, Hakimu Mteite
alikubaliana na hoja ya upande wa mashtaka na kuzuia dhamana, hivyo Sugu na
Masonga walikaa mahabusu katika Gereza Kuu la Ruanda jijini Mbeya kwa siku 24
kabla ya kuachiwa kwa dhamana Februari 9, kwa sharti la kusaini bondi ya Sh5
milioni kila mmoja.
Kabla ya kuanza kutoa ushahidi
Sugu na Masonga wakiongozwa na mawakili wao Mwabukusi, Mwasipu na Yongo
walimkataa Hakimu Mteite kuendelea kusikiliza kesi wakidai ana upendeleo
hivyo hawana imani naye.
Hakimu Mteite aligoma kujiondoa
katika kesi hiyo akisema sababu zilizotolewa na washtakiwa hazina mashiko
kisheria kwa kuwa suala la hakimu kujitoa katika kesi lipo kisheria na kwa
sababu za msingi.
Aliamuru kesi kuendelea kwa Sugu
na Masonga kuanza kutoa ushahidi
Baada ya Hakimu Mteite kugoma
kujitoa katika shauri hilo, mawakili wa utetezi Mwabukusi, Mwasipu na Yongo
walitangaza kujiondoa kuwawakilisha washtakiwa
Kutokana na mawakili hao kujitoa,
Sugu na Masonga waliiomba mahakama kuwapatia muda wa siku 14 ili wajipange
kutafuta mawakili wengine. Ombi hilo lilikubaliwa na mahakama.
Februari 8, Sugu na Masonga
walianza kutoa ushahidi wakiwa na wakili mpya, Peter Kibatala ambaye pia
alimwongoza Mkuu wa Upelelezi Mkoa (RCO) wa Mbeya, Modestus Chambu kutoa
ushahidi.
Rufaa, dhamana zaombwa
Akizungumza baada ya hukumu,
Wakili Kibatala alisema hawaridhiki na hukumu iliyotolewa, hivyo
wamewasilisha maombi ya kukata rufaa pamoja na kuomba dhamana kwa Sugu na
Masonga.
Kibatala alisema kimsingi kulikuwa
na kasoro nyingi katika mwenendo mzima wa kesi hiyo na hata namna hukumu
ilivyotolewa haikuwa sahihi. “Hatujaridha na uamuzi uliotolewa hivyo
tumefuata hatua za kisheria na za kimahakama. Tumekata rufaa, lakini pia
tumeleta maombi ya dhamana kwa wateja wetu wote wawili. Tumeiomba mahakama
kwa haraka iwezekanavyo itupe nakala ya mwenendo wa kesi husika kwa sababu
nakala hiyo ni kitu muhimu katika kukataa rufaa.”
Wakili Kibatala alisema hadi leo
wana imani watakuwa wamepata mwanga zaidi wa maombi ya dhamana na mchakato wa
rufaa watajua unaendeleaje na itasikilizwa lini, lakini akasema kwa mazingira
ya Mbeya yalivyo wanategemea watasikilizwa kwa haraka zaidi.
Kibatala alisema wanazo hoja tisa
ambazo wameziwasilisha katika rufaa yao dhidi ya kesi hiyo.
Imeandikwa na Godfrey Kahango,
Ipyana Samson na Hawa Mathias
|
|
Jinsi saa mbili zilivyotumika kumpeleka Sugu gerezani miezi 5
Reviewed by KUSAGANEWS
on
February 26, 2018
Rating:
Reviewed by KUSAGANEWS
on
February 26, 2018
Rating:


No comments:
Post a Comment