Ripoti ya Twaweza ilivyozua mjadala, sababu za viongozi kupoteza umaarufu



Ripoti ya Taasisi ya Twaweza iliyotolewa juzi jijini Dar es Salaam imeibua mjadala mzito, huku wengi wakihoji sababu ya viongozi wa kuchaguliwa kupoteza umaarufu

Utafiti huo, uliohusisha takwimu zilizokusanywa kutoka kwa watu 1,241 waliohojiwa kutoka Tanzania Bara mwezi Aprili, unaonyesha uungwaji mkono wa Rais John Magufuli umeshuka kutoka asilimia 96 mwaka 2016 mpaka asilimia 55 mwaka 2018, ikiwa ni kiwango cha chini kabisa kuwahi kutokea kwenye historia ya nchi

Hata hivyo, utafiti huo unaonyesha kuwa kama uchaguzi ungefanywa wakati huo, asilimia 55 ya wananchi wangempigia kura. Vilevile umeonyesha bado wananchi kwa kiasi kikubwa wanaendelea kuunga mkono wagombea wa CCM

“Zaidi ya nusu wangewapigia kura wagombea wa CCM wa udiwani (asilimia 51), wabunge (asilimia 51), na urais (asilimia 55). Uungwaji mkono wa CCM kama chama umeendelea kuwa imara kiasi kwenye miaka ya hivi karibuni kukiwa na asilimia 63 ya wananchi wanaosema wako karibu na CCM mwaka 2017 ukilinganisha na asilimia 58 mwaka 2018,” imeonyesha sehemu ya utafiti huo

Wakizungumza katika hafla ya kuwasilisha ripoti hiyo, baadhi ya wachangiaji walielezea sababu za kushuka huko huku pia wakitoa suluhisho

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Vicencia Shule alihusisha kushuka huko na suala la kijinsia, akisema wanawake ambao ndiyo wapigakura wengi wamepuuzwa

Alisema licha ya kupuuzwa, utafiti huo umeonyesha kuamka kwa wanawake hasa kwenye suala la maandamano

“Kwenye suala la maandamano, ufahamu wanawake na wanaume na wanaume kitakwimu hawakupishana sana. Wanaume ni asilimia 43 na wanawake ni asilimia 41. Pamoja na kuogopa vurugu, wanawake wameelewa kwamba yale madai yaliyoleta maandamano ni madai yao,” alisema Dk Shule

Mbali na wanawake, Dk Shule alisema uelewa wa wanaume umeshuka kwenye matatizo ya kijamii, wakati wao ndiyo wameshikilia uongozi wa Dola

“Wanaume wa nchi hii ndiyo waliojitwalia madaraka ya kuongoza nchi bila kujali idadi ya wanawake. Kitu kingine kizuri zaidi ni umaarufu wa Rais unazidi kushuka. Wananchi wameelewa kipi kinatekelezeka na kipi hakitekelezeki,” alisema

Alisema kumekuwepo na tishio la viongozi kupiga wanawake, jambo linalosababisha kushuka kwa kukubalika kwao kwa kuwa wanawake ni wengi katika idadi ya wapiga kura

“Hakuna mtu atakukubali kama unapiga mashangazi, hakuna mtu atakupenda kama unatisha wanawake. Kwa hiyo hii ni ‘wake-up call’ kwa mwenyekiti wa chama, kwamba matendo yake kwa wapigakura ambao wengi ni wanawake, yanathibitisha wazi kuwa umaarufu wake unashuka kwa kuwakosea haki hata kuwanyima fursa ya kushika dola,” alisema
Ripoti ya Twaweza ilivyozua mjadala, sababu za viongozi kupoteza umaarufu Ripoti ya Twaweza ilivyozua mjadala, sababu za viongozi kupoteza umaarufu Reviewed by KUSAGANEWS on July 07, 2018 Rating: 5

No comments: