Wanausalama wa Viwanja vya ndege waimarika


Wanausalama wa viwanja mbalimbali vya ndege nchini, wameiva na kuimarika katika usalama wa vifurushi na mizigo inayosafirishwa kwa njia ya ndege baada ya kufuzu mafunzo yaliyoendeshwa na wakufunzi kutoka Taasisi ya Kimataifa ya Usafiri wa Anga (ICAO).

Wakati akifunga mafunzo hayo Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Viwango cha Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, Bw. Vedastus Fabian kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu, amewataka wahitimu hao kutumia vyema ujuzi walioupata kwa kufanyakazi kwa ufanisi na kuboresha kazi hiyo, ili kuepuka kupitisha mizigo hatarishi kwa usalama wa usafiri wa anga.

“Tunavyojua mfumo wa usafiri wa anga duniani ni moja kwa hiyo tunavyoonesha usalama katika viwanja vyetu vya ndege hapa Tanzania kunajenga imani kubwa kwa mashirika ya ndege na wadau wote wanaofanya shughuli nakutumia viwanja vyetu vya ndege, hivyo tutaongeza wingi wa mizigo,” amesema Bw. Fabian.

Aidha ametoa pongezi kwa wahitimu hao 19 walio Chuo cha Usafiri wa Anga kilichopo katika Jengo la Kwanza la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA-TBI) na kuweza kufaulu vyema mafunzo hayo, ambapo sasa watakuwa na weledi na ufanisi bora katika kazi hiyo.

Amesema TAA inategemea mafunzo hayo yataleta manufaa na sio kuonesha vyeti ukutani kuwa wamehitimu bali ni kuonesha ujuzi walioupata kutasaidia kutambua mizigo na vifurushi vyenye matatizo ya kutishia usalama wa anga na kuongeza uhakika wa safari za anga.
Bw. Fabian pia amesema wanategemea washiriki kufikisha na kusambaza ujuzi huo kwa wanausalama wengine, ambao hawakupata fursa ya kushiriki mafunzo hayo adimu, ili nao waboresha kazi zao.

Wanausalama wa Viwanja vya ndege waimarika Wanausalama wa Viwanja vya ndege waimarika   Reviewed by KUSAGANEWS on May 19, 2018 Rating: 5

No comments: