Usafirishaji dawa za kulevya wawanyima ajira mabaharia


Zaidi ya mabaharia 800 kutoka Zanzibar waliokuwa wakifanya kazi katika meli mbalimbali nje ya Tanzania, wamesimamishwa wakihusishwa na usafirishaji wa dawa za kulevya katika meli hizo.

Hayo yalielezwa mwishoni mwa wiki iliyopita na mkurugenzi wa kampuni ya ubaharia ya Danaos, Ali Mzee Yussuf

Yussuf aliyasema hayo wakati wa mafunzo maalumu yaliyowashirikisha mabaharia mbalimbali visiwani hapa yenye lengo la kupiga vita matumizi na kujihusisha na usafirishaji wa dawa za kulevya

Alisema awali mabaharia kutoka katika kampuni hiyo walikuwa zaidi ya 1,000 lakini kwa sasa wamebaki 200 baada ya wengi wao kukamatwa kwa madai ya matumizi na kusafirisha dawa za kulevya

“Hali hii imekuja baada ya wamiliki wa kampuni za meli husika kuona kuwa mabaharia wetu mara kwa mara hukamatwa kwa kujihusisha na usafirishaji wa dawa za kulevya, hivyo wakaona ni bora kupunguza idadi kutoka kwetu ili kuzinusuru meli zao kuingia katika matata ya usafirishaji dawa hizo,” alisema Yussuf.

Alisema ni ukweli usiopingika kuwa kuna baadhi ya mabaharia kutoka kampuni yao wamekuwa wakikamatwa na dawa za kulevya kutokana na tamaa zao binafsi, lakini kampuni haihusiki

Mkurugenzi huyo alisema kutokana na hali hiyo wamedhamiria kutoa mafunzo kwa baadhi ya mabaharia wa Zanzibar, ili kuwaonyesha hasara watakazozipata wakikamatwa na dawa hizo

“Kwa sasa kupitia chuo chetu cha ubaharia Zanzibar, tumeweka utaratibu maalumu kwa mabaharia wote kutoka hapa lazima wapatiwe elimu ya athari za dawa za kulevya. Mbali na hilo tutafanya uchunguzi maalumu juu yake ili kuona tabia zake kama zinafaa kuwa naye au la, lengo ni kuona kampuni yetu inazidi kupata sifa duniani,” alisema Yussuf

Naye ofisa wa Mamlaka ya Usafiri Baharini (ZMA), Khamis Mohamed Ali alisema kitendo cha mabaharia kujihusisha na usafirishaji dawa za kulevya katika meli hakikubaliki kwa mujibu wa taratibu za kazi.

 Ali alisema kitendo hicho kinaitia aibu kubwa nchi kwa kuonekana inajihusisha na vitendo hatari vya dawa za kulevya.

Alisema wao kama Serikali mara nyingi wamekuwa wakifanya kazi na kampuni hiyo lengo ni kuona wanatekeleza majukumu yao vizuri, ila ni jambo la kushangaza baadhi yao wamekuwa wakijihusiha na usafirishaji wa dawa za kulevya.

Usafirishaji dawa za kulevya wawanyima ajira mabaharia Usafirishaji dawa za kulevya wawanyima ajira mabaharia Reviewed by KUSAGANEWS on May 13, 2018 Rating: 5

No comments: