Mwili wa mwanafunzi wa Muhas aliyefia chumbani ulivyobainika


Ofisa habari wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (Muhas), Hellen Mtui ameeleza namna walivyobaini kuwa mwanafunzi wa mwaka wa tatu chuoni hapo, Edward Kahitwa amefariki dunia

Kahitwa aliyekuwa akisoma shahada ya famasia chuoni hapo, mwili wake uligundulika Mei 19 katika chumba namba 65 kilichopo Hosteli ya Kagera alikokuwa akiishi peke yake

Hellen alisema jana kuwa kwa takriban siku tatu, wahudumu wa usafi waligonga mlango wa chumba ili wafanye usafi lakini hawakufunguliwa

Alisema hali hiyo haikuwa ya kawaida kwa wahudumu hao kutofunguliwa mlango na pia kulikuwa na harufu iliyokuwa ikitoka ndani

Ofisa huyo alisema wahudumu hao waliingiwa hofu na hivyo kwenda kuwaita walinzi walioamua kuvunja mlango. Baada ya mlango kuvunjwa, walikuta mwili wa Kahitwa ukiwa kitandani na baada ya hapo walitoa taarifa polisi

Alisema askari walifika na kuuchukua mwili wa marehemu kwa ajili ya uchunguzi

“Kahitwa ni mtu wa Bukoba, lakini tumeambiwa ana ndugu yake Ununio, Dar es Salaam. Tunatarajia kumuaga kesho (leo) asubuhi na baadaye mwili utasafirishwa kwenda Bukoba ambako tunaambiwa ndiko mama yake yupo,” alisema Hellen

Chanzo cha kifo cha mwanafunzi huyo bado hakijajulikana, polisi wakieleza kuwa wanaendelea na uchunguzi

“Tumepokea taarifa za kifo cha mwanafunzi huyo lakini chanzo cha kifo chake bado hakijafahamika. Mwili wake umehifadhiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili,” alisema Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Salum Hamduni

Jitihada za kuwapata wanafunzi wanaoishi jirani na chumba cha Kahitwa ziligonga mwamba jana baada ya Rais wa Serikali ya wanafunzi Muhas (Muhasso), Geovanni Kihaga kuwazuia waandishi wa habari akisema hawaruhusu mtu yeyote kuzungumzia suala hilo
Alisema ibada ya kuaga mwili wa marehemu itafanyika leo katika kanisa lililopo Muhimbili

“Tunapata ugumu kulizungumzia suala hili kwa sababu kuna utata, wapo wanaosema marehemu ni mtu wa Iringa, wengine wanasema Morogoro na wengine wanasema Bukoba. Familia yake ndiyo itatupa mwongozo mzuri,”
Mwili wa mwanafunzi wa Muhas aliyefia chumbani ulivyobainika Mwili wa mwanafunzi wa Muhas aliyefia chumbani ulivyobainika Reviewed by KUSAGANEWS on May 21, 2018 Rating: 5

No comments: