Ofisa mifugo ajiua kwa kujitundika kamba kwenye zizi la Ng"ombe

Misungwi. Ofisa Mifugo wa Wilaya ya Nyamagana jijini Mwanza, Michael Fundo (57), amefariki dunia kwa kunywa sumu kabla ya kujitundika kwa kamba ndani ya zizi la ng’ombe nyumbani kwake wilayani Misungwi

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo linalodaiwa kusababishwa na msongo wa mawazo kutokana na Michael kuwa na ugomvi wa muda mrefu wa kifamilia

Mmoja wa wanafamilia aliyezungumza kwa sharti la kutotajwa jina, amesema ugomvi huo ulitingisha pia ndoa yake

“Kabla ya kujinyonga kwa kamba, alikunywa sumu aliyoona inamchelewesha,” amesema Kamanda Msangi

Licha ya kuwa mtumishi wa Halmashauri ya Manispaa ya Nyamagana ambayo kwa pamoja na Ilemela zinaunda Jiji la Mwanza, Michael alikuwa akiishi wilaya jirani ya Misungwi

Mtumishi wa ndani wa familia hiyo, John Anthony (23) amesema kabla ya kuchukua uamuzi wa kujitoa uhai, alifanya hesabu ya kikundi cha kuweka na kukopa ambacho alikuwa mtunza fedha na kukabidhi nyaraka na fedha zote akielekeza zikabidhiwe kwa wana kikundi wenzake

“Marehemu pia aliandika wasia ukihusisha mali pamoja na madeni anayodai na kudaiwa, jambo lililotutia mashaka ni kwa nini anafanya hivyo,” amesema Anthony

Kwa mujibu wa mmoja wa wanakikundi, leo Aprili 28, walipanga kugawana fedha walizokusanya. 
Ofisa mifugo ajiua kwa kujitundika kamba kwenye zizi la Ng"ombe Ofisa mifugo ajiua kwa kujitundika kamba kwenye  zizi la Ng"ombe Reviewed by KUSAGANEWS on April 28, 2018 Rating: 5

No comments: