Askari
wanaoshiriki doria kuzuia uvuvi haramu wilayani Sengerema, wamedaiwa kuwakamata
na kuwapiga wananchi wakiwamo wanafunzi wakiwashinikiza kuonyesha zilikofichwa
zana haramu.
Tuhuma hizo zilitolewa
juzi na wananchi wakiongozwa na diwani wa Kahumulo, Mashauri Nzwagi wakati wa
kikao cha pamoja kilichoitishwa na mkuu wa wilaya hiyo, Emmanuel Kipole kwa
lengo la kusikiliza na kutatua kero za wananchi.
Kikao
hicho kilihudhuriwa na wafanyabishara wa samaki, wavuvi, wananchi na maofisa
wanaoshiriki doria hizo. “Hawa maofisa wanaoshiriki doria wanawakamata na
kuwapiga hovyo wananchi bila sababu za msingi. Wapo wananchi wameumizwa,”
alisema Nzwagi.
Aliwataja wanafunzi
wawili ndugu wa Sekondari ya Kahumulo, Kelvin Zambona na Mzilya Zambona kuwa ni
miongoni mwa waliopigwa na kujeruhiwa na askari hao wa doria waliokutwa
wakitoka tuisheni.
Wakitoa ushuhuda,
wanafunzi hao walisema askari hao waliwakamata saa 11:00 jioni ya Aprili 22,
wakiwa njiani wakitoka shule na kuwataka waonyeshe baba yao alikofichwa zana
haramu za uvuvi.
“Baada kuwajibu kuwa
baba yetu hana zana haramu za uvuvi, wala hatujui kama anashiriki vitnedo
hivyo, ghafla askari likaanza kutupiga,” alisema Kelvin.
Naye
mkuu wa kikosi cha doria wilayani Sengerema kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi,
Wenceslaus Luhasile aliahidi kuchunguza tuhuma hizo na kuonya kuwa hatua za
kisheria na nidhamu zitachukuliwa iwapo itathibitika kuwa askari hao wamehusika
na vitendo vinavyokiuka sheria.
Askari doria uvuvi haramu wachongewa kwa DC
Reviewed by KUSAGANEWS
on
April 30, 2018
Rating:
Reviewed by KUSAGANEWS
on
April 30, 2018
Rating:


No comments:
Post a Comment