FAMILIA YA AKWELINA YAOMBA MSAADA KWA WAZIRI NDALICHAKO


Siku mbili baada ya Waziri wa Elimu, Profesa Joyce Ndalichako kuahidi kumsomesha Angela Akwilini, mdogo wa marehemu Akwilina aliyekuwa mwanafunzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), familia hiyo imetoa ombi lingine kwa Serikali.

Msemaji wa familia hiyo, Dismas Shirima akizungumza na Mwananchi jana alisema, “Nampongeza waziri kwa kuona umuhimu wa kuziba pengo la Akwilina kwa kumsomesha mdogo wake Angela aliyekuwa akitegemewa kwa kiasi kikubwa katika familia.”

Shirima pia alimuomba Waziri Ndalichako kumsomesha ndugu mwingine wa Akwilina aliyeacha shule akiwa kidato cha tatu kwa kukosa mahitaji ya shule

“Waziri akifanya hivyo atakuwa amepunguza machungu kwa familia hii maskini,” alisema.

Mtoto huyo, Yulia Akwilini (19) alikuwa akisoma Shule ya sekondari Maki na ameahidi kwamba akipata nafasi ya kuendelea na masomo atasoma kwa bidii ili kutimiza ndoto zake zilizoishia njiani

“Natamani nami nipate nafasi ya kuendelea na masomo, natamani nifike na chuo kikuu kama dada yangu. Nilitamani nisome lakini kutokana na familia yangu kuwa duni niliishia njiani japo dada yangu alijitahidi kunisomesha lakini ndiyo hivyo ameenda,” alisema Yulia aliyeacha shule akiwa kidato cha tatu mwaka 2016.

Akwilina aliyekuwa mwanafunzi wa mwaka wa kwanza NIT, alifariki dunia Februari 16 kwa kupigwa risasi wakati polisi wakitawanya maandamano ya wafuasi wa Chadema waliokuwa wanaelekea ofisi ya msimamizi wa uchaguzi jimbo la Kinondoni kudai hati za viapo vya mawakala wao

Wakati wa mazishi ya Akwilina yaliyofanyika Februari 23, Olele wilayani Rombo, Kilimanjaro, waziri Ndalichako aliahidi kumsomesha Angela (16) anayesoma kidato cha tatu katika sekondari ya Kata ya Maki iliyopo tarafa ya Mashati wilayani Rombo hadi pale atakapofikia kiwango cha elimu atakachoona kinafaa.

Profesa Ndalichako alisema Akwilina alikuwa akitumia fedha zake za kujikimu kumsomesha mdogo wake, hivyo kuanzia sasa yeye ndiye atakayetekeleza jukumu hilo na kuhakikisha binti huyo anapata elimu bora.

Angela akizungumzia ahadi ya waziri Ndalichako alisema ameipokea kwa furaha

“Dada alijitahidi kwa kadri alivyoweza ili nisome lakini ndiyo hivyo Mungu kamchukua inaniuma, niliona ndoto yangu ya elimu ndiyo imefika mwisho. Nikichukuliwa na waziri nitapambana kwa kadri niwezavyo hadi nimpite hata dada yangu alipofikia,” alisema Angela.

Alimzungumzia pia Yulia akisema, “Nitafurahi kama waziri atamsaidia dada yangu aliyeacha shule akiwa kidato cha tatu, dada yetu (Akwilina) alikuwa ni tegemeo letu,” alisema.

Kuanua tanga Shughuli ya kumaliza msiba, itafanyika leo ili kuiwezesha familia kuendelea na mambo mengine.

Shirima alisema shughuli zote zilizopangwa na Serikali katika msiba huo zilifanyika vizuri na kama kuna changamoto zilizojitokeza ni ndogondogo.









FAMILIA YA AKWELINA YAOMBA MSAADA KWA WAZIRI NDALICHAKO FAMILIA YA AKWELINA YAOMBA MSAADA KWA WAZIRI NDALICHAKO Reviewed by KUSAGANEWS on February 26, 2018 Rating: 5

No comments: