MBUNGE WA NGORONGORO MAMBO MAZITO WANANCHI WANATESEKA NITASHIKA SHILINGI YA WAZIRI MKUU

MBUNGE wa Ngorongoro, Emmanuel Ole Shangai ameitaka serikali kuja na kauli moja inayotaka wakazi wote wa eneo la Ngorongoro kuondoka kwa lazima kuliko kuendelea kufanya alichokiita kuwawekea vikwazo katika huduma muhimu za kijamii, ikiwamo upatikanaji maji safi na salama.

Shangai alitoa kauli hiyo bungeni wakati akichangia mapatio na mwelekeo wa kazi za serikali na makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa mwaka ujao wa fedha.

Amesema kuwa kwa sasa hali ya wakazi wa eneo la Ngorongoro imeendelea kuwa ngumu kutokana na vikwazo wanavyowekewa.

Mbunge huyo amesema serikali inatakiwa itoe tamko kwa wananchi zaidi ya 108,000 walioamua kubaki katika Tarafa ya Ngorongoro baada ya wale wengine 7,000 kuhamia Msovera na wao watoke kwa lazima kwa kuwa huduma nyingi zimefungwa kwa sasa.

Ametaja huduma zilizofungwa kwa wananchi hao kuwa ni pamoja na zaidi ya shule 27 za msingi katika tarafa hiyo ambazo aliliambia Bunge kuwa zote zimezuwa kujenga wala kukarabati vyoo, hali inayosababisha walimu na wanafunzi kujisaidia porini.

Mbunge huyo pia amesema kuna shule ya msingi ya bweni imesitishiwa huduma ya maji, hali inayowalazimu wananchi kufuata huduma ya maji mtoni na kuhatarisha maisha yao.

“Kwanini tunafanya hivi? Kila mwananchi ana haki ya kupata huduma na zoezi la kuhama lilikuwa la hiari na Waziri Mkuu alipozungumza na wananchi alithibitisha hilo. Iweje sasa tuanze kuwawekea vikwazo vya maendeleo?" Shangai amehoji.

Amesema ni zaidi ya miaka mitatu sasa wananchi hawapati huduma stahiki zikiwamo huduma za afya ambazo zimekuwa hafifu na kuhoji wananchi wameikosea nini serikali kwa kuwa wako katika eneo hilo kisheria.

Mbunge huyo amesema licha ya jimbo kupata maendeleo mbalimbali ikiwamo kujengwa shule za sekondari na msingi kutokana na jiografia ya mazingira ya wanyama katika shule hizo, wanafunzi hawatafaidi kutokana kutokuwa na mabweni pamoja na nyumba za walimu ili wanafunzi wapate huduma ipasavyo.

“Wakati wa hotuba ya kuhitimisha hoja hii, mniambie kwamba serikali ina mpango gani na wananchi wa Tarafa ya Ngorongoro? 

Isitoshe kwenye geti la Ngorongoro wananchi wakirudi jioni hawaruhusiwi kuingia mpaka wawe na vitambulisho vya wapigakura ilhali wapo baadhi ya vijana wenye umri wa chini ambao wanawalazimisha kwenda polisi kuchukua taarifa inayowatambulisha,” amesema.

Mbunge Shangai pia amesema hata wafanyabiashara wa mifugo wanazuiwa kufanya shughuli zao, wakitakiwa kubeba ng’ombe kwa malori ilhali hakuna miundombinu ya barabara ya kupitisha magari hayo.

“Kama imefika wakati ni bora tuwaambie kwamba hawahitajiki katika eneo hilo ili waondoke kuliko kuendelea kuwapa mateso maana upo pia mradi wa elimu wa wanafunzi kusomeshwa vyuo vikuu na vyuo vya kati, lakini wanafunzi zaidi ya 154 waliopitishwa na Baraza la Wafugaji wamesitishiwa ufadhili hali inayosababisha ongezeko la watoto wa kike kujihusisha na vitendo vibaya vya kujiuza ili kupata chochote,” amesema.

Vilevile, amesema wafanyabiashara wameanza kugomea minada baada ya serikali kupitia halmashauri kuongeza kodi katika mifugo ambapo kwa mbuzi imeongezeka kutoka Sh. 2,500 hadi 8,000 huku madiwani, Mwenyekiti wa Halmashauri wakiwa hawajui na ushuru huo unakusanywa kwa kutumia wanajeshi.

Katika hotuba yake bungeni wiki iliyopita wakati wa kuwasilisha hoja hiyo, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema kuwa atika jitihada za kulinda bioanuai ya hifadhi na kuboresha maisha ya wananchi wanaoishi ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro, serikali imeendelea kuwahamisha kwa hiari wananchi kutoka ndani ya eneo la hifadhi kwenda katika maeneo yaliyotengwa na serikali huko Msomero wilayani Handeni, Saunyi (Kilindi), Kitwai (Simanjiro) na maeneo mengine ambayo wananchi wamechagua. 

Waziri Mkuu amesema kuwa katika awamu ya pili, jumla ya nyumba 5,000 zinajengwa katika maeneo ya Msomera (2,500), Saunyi (1,000) na Kitwai (1,500) ambapo katika kipindi cha kuanzia Julai 2023 hadi 21 Februari 2024, jumla ya nyumba 700 zimekamilika na nyumba 1,800 ziko katika hatua mbalimbali za ujenzi. 

"Katika kipindi cha Julai 2023 hadi Februari 2024, jumla ya kaya 491 zenye watu 3,451 na mifugo 14,599, zimehama kwa hiari na hivyo kufanya jumla ya kaya zilizohamia tangu kuanza kwa zoezi hili Julai 2022 kufikia 1,042, ikijumuisha jumla ya watu 6,461 na mifugo 29,919," Majaliwa amefafanua.

 

MBUNGE WA NGORONGORO MAMBO MAZITO WANANCHI WANATESEKA NITASHIKA SHILINGI YA WAZIRI MKUU MBUNGE WA NGORONGORO MAMBO MAZITO WANANCHI WANATESEKA NITASHIKA SHILINGI YA WAZIRI MKUU Reviewed by KUSAGANEWS on April 09, 2024 Rating: 5

No comments: