Mtoto afariki kwa kuparuliwa na paka Kilimanjaro

Mtoto wa miaka mitatu, mkazi wa Longuo, Kilimanjaro, amefariki dunia juzi baada ya kuparuliwa na paka

Kifo cha mtoto huyo, kinafanya idadi ya watu waliokufa kutokana na kuumwa na wanyama aina ya mbwa na paka wilayani Moshi kufikia wanne katika kipindi cha siku 30

Bila kutaja jina, Ofisa Afya wa Mkoa wa Kilimanjaro, Jornas Mcharo alisema mtoto huyo alifikishwa hospitali, Aprili 2 akiwa na dalili za kichaa cha mbwa

Akieleza ni kwa nini mtoto huyo alionekana kuwa na virusi vya rabbies, (kichaa cha mbwa) wakati ameparuliwa na paka, Mcharo alisema kwa kawaida ugonjwa wa kichaa cha mbwa unatokana na kukwaruzwa na wanyama wenye damu za moto. Alisema imezoeleka kuitwa kichaa cha mbwa lakini husababishwa na wanyama wote wenye virusi hivyo

“Wanyama hao ni wale wenye virusi kama mbwa, paka, panya, mbweha na popo au hata binadamu mwenye maambukizi ya virusi hivyo,” alisema

Alisema huo ni miongoni mwa magonjwa yanayoambukiza binadamu na wanyama yanayojulikana kama (zoonotic diseases

Kuhusu mtoto huyo, Mcharo alisema baada ya matibabu yake kushindikana katika vituo vya afya, alihamishiwa Hospitali ya Rufaa ya KCMC lakini alipoteza maisha juzi wakati akipatiwa matibabu

Alisema mtoto huyo baada ya kuparuliwa na paka, hakupata matibabu mapema hadi baada ya wazazi wake kuona hali yake inakuwa mbaya, ndipo wakampeleka hospitali. Ilibainika kuwa familia ya mtoto huyo inafuga paka saba

“Kitu cha kushangaza kidogo, katika mtaa huo wa Longuo A, familia nyingi zinafuga paka zaidi ya watano, sasa hii ni hatari kwa kuwa hawajachanjwa na watoto wanacheza na paka bila kujua kama kuna hatari yoyote inayoweza kutokea,” alisema

Ofisa Afya Manispaa ya Moshi, Mgeta Sebastian alisema kati ya Januari hadi sasa, watu 201 wameng’atwa na mbwa katika manispaa hiyo, huku mbwa 113 wakipewa chanjo na 204 wakiuawa

Alizitaka familia kuwapa chanjo wanyama wafugwao majumbani na kuwapeleka hospitali mapema watu wanaojeruhiwa na wanyama hao.
Mtoto afariki kwa kuparuliwa na paka Kilimanjaro Mtoto afariki kwa kuparuliwa na paka Kilimanjaro Reviewed by KUSAGANEWS on April 05, 2018 Rating: 5

No comments: