MKUU WA CHUO CHA UHASIBU ARUSHA AHUKUMIWA KIFUNGO


Professor Johannes Mbusiro Monyo Mkuu wa Chuo Cha Uhasibu Arusha (IAA) amehukumiwa kifungo cha nje cha mwaka mmoja baada ya kupatikana na hatia kwa makosa ya rushwa. Hii ilikuwa baada ya kusikilizwa kwa kesi iliyokuwa inamkabili toka mwaka 2014.

Hukumu hiyo ilitolewa na Mhe. Devota Msofe katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, Mahakama iliridhika na ushahidi uliowasilishwa na upande wa Jamhuri hivyo tarehe 29/04/2016 mshitakiwa alikutwa na hatia kwa makosa yote aliyoshitakiwa nayo. Aidha, katika kipindi hicho akiwa anatumikia adhabu hiyo hatakiwi kufanya kosa lolote la jinai. 

Mnamo tarehe 08.02.2013 Ofisi ya TAKUKURU (M) Arusha ilipokea tuhuma kuhusiana na Professor Johannes Mbusiro Monyo Mkuu wa Chuo Cha Uhasibu Arusha (IAA). Professor Johannes Mbusiro Monyo alikuwa anatuhumiwa kwa kujihusisha na vitendo vya rushwa kinyume na sheria namba 11/2007. 

Taarifa hiyo ilibainisha kwamba mtajwa alijihusisha na vitendo vya rushwa na kufanikisha kuwapatia ajira za kudumu watumishi wanane (8) katika chuo hicho wakati akijua kwamba watumishi hao hawakuwa na sifa. Katika kuthibitisha tuhuma dhidi ya mtuhumiwa, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana Rushwa ilianzisha uchunguzi na baada ya kukamilisha uchunguzi huo iliwasilisha jalada kwa Mkurugenzi wa Mashtaka kisha kilitolewa kibali cha mtuhumiwa kufikishwa mahakamani kwa kosa la Matumizi Mabaya ya Madaraka. 

TAKUKURU (M) wa Arusha baada ya kukamilisha uchunguzi tarehe 31/07/2014 ilimfikisha mtuhumiwa mahakamani na kufunguliwa shauri la jinai namba 15630 akikabiliwa na makosa 16 ya matumizi mabaya ya madaraka kinyume na kifungu cha 31 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Namba 11 ya mwaka 2007. 

Makosa nane ya kwanza kati ya makosa 16 yalikuwa ni ya kujihusisha na vitendo vya rushwa kwa kutumia madaraka yake vibaya hivyo kuwaingiza katika utumishi wa umma watumishi nane bila ya kupata kibali kutoka kwa Katibu Mkuu – Utumishi. Watumishi hao ni wafuatao: Pamela Dismass Maboko, Samsoni Laurance Mbarya, Mawazo Elias Ndaro, Juma Babu Nyarutu, Lilian Anselim Ngowi, Godfrey Daudi Mollel, Musa Ramadhani Maiki na Salim A. Shaban.

Aidha, makosa nane ya pili kati ya makosa 16, yalikuwa ni mtuhumiwa kujihusisha na vitendo vya rushwa kwa kutumia madaraka yake vibaya kwa kuwaingiza katika utumishi wa umma watumishi hao hao nane ilihali akijua fika kwamba wahusika hawakuwa na elimu ya kidato cha nne kiwango ambacho ni cha chini kabisa kinachohitajika kwa Mtumishi wa Umma kuajiriwa. Kwa kufanya hivyo mshitakiwa alikwenda kinyume na Sheria ya Utumishi wa Umma Namba 02 ya mwaka 2002 kama ilivyofanyiwa marekebisho mara kwa mara. 

TAKUKURU Mkoa wa Arusha inawashukuru wananchi kwa ushirikiano wanaouonesha kwa kuendelea kutoa taarifa za vitendo vya rushwa. Aidha, inawatahadharisha watumishi wote wa Umma na binafsi kuzingatia maadili wakati wa utekelezaji wa majukumu yao kwani TAKUKURU haitasita kuchukua hatua stahiki dhidi ya yeyote atakayejihusisha na vitendo vya rushwa.
IMETOLEWA NA
JUVENTUS M. BAITU
MKUU WA TAKUKURU (M) ARUSHA
5/5/ 2016
MKUU WA CHUO CHA UHASIBU ARUSHA AHUKUMIWA KIFUNGO MKUU WA CHUO CHA UHASIBU ARUSHA AHUKUMIWA KIFUNGO Reviewed by KUSAGANEWS on May 06, 2016 Rating: 5

No comments: