Wakili aeleza sababu za kujitoa kesi ya Mbowe


Wakili Jeremiah Mtobesya amejitoa kuwawakilisha katika kesi viongozi tisa wa Chadema, akiwamo mwenyekiti Freeman Mbowe akisema anaona haki haitatendeka.

Mtobesya alijiondoa katika kesi hiyo iliyopo Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri

Alifikia uamuzi huo baada ya Mahakama kutoa uamuzi wa kutupilia mbali maombi ya wateja wake ya kutaka kesi hiyo ya jinai namba 112/2018 iahirishwe ili kusubiri kusikilizwa maombi na rufani iliyopo Mahakama ya Rufaa.

 Washtakiwa wamewasilisha katika Mahakama ya Rufaa maombi wakitaka kesi ya msingi iliyopo Kisutu isitishwe usikilizwaji hadi rufaa ya kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu wa kutupilia mbali maombi ya marejeo namba 126/2018 itakaposikilizwa na uamuzi kutolewa

Katika Mahakama Kuu, washtakiwa waliiomba irejee mwenendo wa kesi na uamuzi uliotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu

Jana, baada ya Hakimu Mashauri kuyatupilia mbali maombi ya washtakiwa aliamuru wasomewe maelezo ya awali ya kesi inayowakabili

Wakili Mtobesya alieleza kuwa kesi ilipangwa kwa ajili ya kutajwa na uamuzi ulitolewa

Alisema hakubaliani na ombi la upande wa mashtaka la kuwasomea washtakiwa maelezo ya awali
Wakili Mtobesya aliieleza Mahakama kuwa anajiondoa katika kesi kwa sababu anaona kwa namna mwenendo wa kesi unavyokwenda haki haitatendeka

Kwa kauli hiyo, Mtobesya alibeba begi lake na kuondoka ndani ya ukumbi namba moja wa Mahakama ambako kesi ilikuwa ikiendeshwa

Aliwaacha washtakiwa wakiwa hawana wakili mahakamani kwa kuwa wakili mwingine anayewawakilisha, Peter Kibatala hakuwapo

Hakimu Mashauri aliwaeleza washtakiwa kwa kuwa hawakuwa na wakili mwingine mahakamani, anaahirisha kesi hadi Agosti 27 watakaposomewa maelezo ya awali

Hakimu Mashauri katika uamuzi wa kutupilia mbali maombi ya washtakiwa, alisema kifungu cha sheria ya mwenendo wa mashauri ya jinai kilichotumika kuwasilisha maombi hayo, hakiipi Mahakama mamlaka ya kuahirisha kesi kusubiri uamuzi wa Mahakama ya Rufaa

Alisema hata kama kifungu hicho kingekuwa kinaipa Mahakama mamlaka ya kufanya hivyo, basi isingefanya hivyo kwa sababu ilishatoa uamuzi mara kadhaa kutokana na maombi mbalimbali ya utetezi na kuyatupilia mbali, hivyo haiwezi kula matapishi yake

Baada ya uamuzi kutolewa, wakili wa Serikali mkuu, Faraja Nchimbi alisema kesi hiyo ilipangwa kwa ajili ya kutajwa, na kwa kuwa uamuzi umeshatolewa aliiomba Mahakama iridhie washtakiwa wasomewe maelezo ya awali. Ombi hilo lilipingwa na Mtobesya

Hakimu Mashauri alisema ni kweli kesi ilipangwa kwa ajili ya kutajwa kusubiri uamuzi ambao alishautoa, hivyo haoni haja ya kuahirisha kusomwa kwa maelezo ya awali

Alisema usomaji wa maelezo hayo hauhitaji maandalizi, hivyo aliamuru upande wa mashtaka kuwasomea washtakiwa hao

Wakili Kibatala alipowasilisha maombi awali, alidai Mahakama hiyo ina mamlaka ya kuiahirisha kesi ya jinai namba 112/2018 kwa kipindi kisichozidi siku 15 iwapo mshtakiwa atakuwa ndani na kisichozidi siku 30 iwapo mshtakiwa au washtakiwa watakuwa nje kwa dhamana

Wakili Nchimbi alidai kuwa maombi hayo ya utetezi yanakosa baraka za kisheria na hata miguu ya kisheria ya kusimama mbele ya Mahakama hiyo

Aliiomba Mahakama itupilie mbali maombi yaliyowasilishwa na upande wa utetezi kwa sababu yanakosa msingi wa kisheria

Alidai maombi ya upande wa utetezi yanalenga kuchelewesha kesi na hakuna kipya kilichowasilishwa mahakamani. Mbali na Mbowe washtakiwa wengine katika kesi hiyo ya jinai ni naibu katibu mkuu wa Chadema –Zanzibar, Salum Mwalimu na naibu katibu mkuu –Bara, John Mnyika ambaye pia ni mbunge wa Kibamba.

 Wengine ni wabunge wa Tarime Vijijini, John Heche; Halima Mdee (Kawe), Ester Bulaya (Bunda), Mchungaji Peter Msigwa (Iringa Mjini), Esther Matiko (Tarime Mjini) na katibu mkuu wa chama hicho, Dk Vincent Mashinji

Washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka ya kula njama, kufanya mkusanyiko wenye ghasia, kuhamasisha hisia za chuki, kushawishi hali ya kutoridhika, uchochezi na kushawishi utendaji jinai

 Washtakiwa wanadaiwa kutenda makosa hayo kati ya Februari Mosi na Februari 16 jijini Dar es Salaam

Wakili aeleza sababu za kujitoa kesi ya Mbowe Wakili aeleza sababu za kujitoa kesi ya Mbowe Reviewed by KUSAGANEWS on August 23, 2018 Rating: 5

No comments: