Daktari aeleza Consolata alivyofariki baada ya mwenzake


Dk Faith Kundy aliyekuwa akiwahudumia pacha Maria na Consolata katika Hospitali ya Mkoa wa Iringa ameeleza jinsi Consolata alivyofariki dunia kati ya dakika 10 hadi 15 baada ya mwenzake kufariki.

“Wakati tunampa Maria huduma ya kwanza na namna alivyokuwa anatapatapa, Consolata alianza kuhisi hali hiyo ndio maana alikuwa akinisukuma na kusema tuache, tuache, tuache na nilikuwa nawaambia pumua... pumua... pumua... niliwasisitiza hivyo,” amesema Dk Kundy

Ameeleza kuwa katika kuungana kwao kuna viungo vilivyokuwa pamoja

“Anaweza kula Consolata na Maria akasema ameshiba na hata suala la maumivu ataanza kulalamika Consolata na baada ya muda mfupi Maria analalamika,” amesema

Daktari huyo ameeleza kuwa tangu walipowapokea pacha hao kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, hawakuwa kwenye hali nzuri kwa sababu Maria alikuwa akitumia oksijeni kupumua

“Kwa hiyo walikuwa chini ya uangalizi na tulikuwa tunaangalia hali zao na kama kuna tatizo basi tunawasaidia,” amesema

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa, Museleta Nyakiroto alipoulizwa kuhusu iwapo mmoja angeendelea kuwa hai kwa muda mrefu, amesema pacha hao walikuwa na mshipa mmoja mkubwa wa damu uliokuwa ukiwasaidia wote wawili

Dk Nyakiloto aliwaeleza waandishi wa habari Jumamosi, Juni 2 kuwa pacha hao walifariki dunia wakipatiwa matibabu katika chumba cha uangalizi maalumu (ICU).
“Tangu wafikishwe hospitalini hatukuwahi kuona wakibadilika kiafya kiasi kile. Jana (juzi) hali yao ilikuwa tofauti sana. Maria ndiye alianza kufariki na baada ya dakika 10 alifuata Consolata,” alisema

Daktari aeleza Consolata alivyofariki baada ya mwenzake Daktari aeleza Consolata alivyofariki baada ya mwenzake Reviewed by KUSAGANEWS on June 04, 2018 Rating: 5

No comments: