Jeshi la Polisi mkoani Mara linaendelea na
msako dhidi ya watu wanaotuhumiwa kuhusika na mauaji ya mfanyabiashara na
mmiliki wa kampuni ya mabasi ya Super Sami, Josia Mzuri maarufu kwa jina la
Samson ambaye mwili wake ulikutwa kwenye viroba ndani ya Mto Ndabaka mpakani
mwa wilaya za Bunda na Busega
Akizungumza kwa njia ya simu jana, kamanda
wa polisi Mkoa wa Mara, Jaffari Mohamed alisema pamoja na msako dhidi ya
watuhumiwa wengine, pia jeshi hilo linaendelea kuwahoji watu wanne wanaoshikiliwa
kuhusiana na tukio hilo
Kamanda Mohamed alitoa wito kwa watu wenye
taarifa zitakazosaidia kuwanasa wahusika au kufanikisha ushahidi dhidi ya
watuhumiwa wanaoshikiliwa kujitokeza kuziwasilisha polisi
“Suala hili linahitaji uchunguzi wa kina si
tu kubaini na kuwanasa wahusika, bali pia kupata ushahidi wa kina unaotosheleza
kuwatia hatiani. Tunaomba raia wema washirikiane na polisi kukamilisha jukumu
hilo,” alisema
Kauli ya kamanda huyo inakuja baada ya zaidi
ya wiki moja tangu mwili wa Mzuri ukutwe mtoni na kuzikwa nyumbani kwake mtaa
wa Majengo ya Chini mjini Magu mkoani Mwanza
Baadhi ya wafanyabiashara wenzake na Josia
walielezea kuingiwa na hofu juu ya usalama wao na kutokana na kutojulikana
sababu za mauaji hayo
Hofu ya wafanyabiashara na wamiliki wa
mabasi ya abiria mkoani Mwanza ilitolewa na Joseph Kasheku ‘Msukuma’
alipozungumza kwa niaba ya wenzake siku ya mazishi Machi 16 na kuviomba vyombo
vya dola kuchunguza suala hilo ili kuwabaini wahusika na sababu za kufanya
hivyo
“Mauaji haya yameibua hofu na wasiwasi
mwingi miongoni mwetu wafanyabiashara ya usafirishaji wa abiria mkoani Mwanza
kwa sababu hatujui kwa nini mwenzetu katekwa na kuuawa wala hatuelewi nani
atafuata miongoni mwetu,” alisema Msukuma ambaye pia ni Mbunge wa Geita
Vijijini
Josia alitoweka tangu Februari 27, siku moja
baada ya kushiriki kikao cha kamati ndogo ya Chama cha Wamiliki wa Mabasi
Tanzania (Taboa) Mkoa wa Mwanza kilichofanyika jijini Mwanza Februari 26
Machi 9, gari lake lilikutwa likiwa
limeteketezwa kwa moto ndani ya eneo la Hifadhi ya Taifa ya Serengeti mkoani
Mara, siku tano kabla ya mwili wake kukutwa ndani ya maji katika Mto Ndabaka
ukiwa umefungwa kwenye viroba
Akizungumzia tukio hilo, ofisa habari wa
Taboa, Mustapher Mwalongo alilitaja kuwa ni la kusikitisha na kuogofya na
kuviomba vyombo vya dola kufanya uchunguzi ili kuwanasa wahusika, huku mmoja wa
mawakala wa tiketi za mabasi wa Kituo Kikuu Nyegezi, Leonard Joseph akisema
kifo hicho kilipokewa kwa mshtuko na wadau wa usafirishaji kutokana na
mazingira yake na ukaribu wa Josia na watu waliomzunguka.
POLISI WAENDELEA NA MSAKO WA WATU WALIOFANYA MAUAJI
Reviewed by KUSAGANEWS
on
March 25, 2018
Rating:
No comments:
Post a Comment