SABABU YA WANAFUNZI KUFANYA VIBAYA KATIKA ELIMU DODOMA NI WAZAZI

Utafiti uliofanywa na wahadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) kuhusu sababu za mkoa wa Dodoma kufanya vibaya katika elimu umeanika mambo kadhaa ikiwemo wazazi kuwashawishi watoto wao wasifanye vizuri katika mitihani yao.

Akizungumza katika mkutano wa wadau wa elimu mkoani hapa leo Februari 20, 2018 mmoja wa jopo la wahadhiri hao,  Dk. Fransic William amesema baadhi ya wazazi wamekuwa wakiwashawishi watoto wao kuandika makorokoro katika mitahani yao ya Taifa

“Katika baadhi ya shule tulikuta wanafunzi walikuwa wanafanya vizuri katika mitihani mingine ya ndani ya shule lakini ikija katika mitihani ya Taifa wanafanya vibaya,”amesema Dk William.

Amesema pia katika utafiti huo, walibaini pia kuna shule zina madarasa matatu tu lakini wanafunzi wapo hadi darasa la saba na hivyo kulazimika wengine kusoma na kukaa chini ardhini kwa ukosefu wa vyumba vya madarasa na madawati

“Hao unaowaona wamelala hapo chini ndio wanafanya mitihani hapo. Unakuta shule ina walimu wawili na wanafunzi 700 kwa  wiki mwalimu

anavipindi  60 hapo unadhani anaweza kumudu kweli,” amehoji.

Amesema pia tatizo jingine ni wanafunzi kulazimika kutembea umbali mrefu kutoka na kurudi nyumbani ambapo kuna watoto wanatembea umbali wa kuanzia kilometa tano hadi 18 kwa siku.

Ametoa mfano wa shule mojawapo kati ya watoto 9 waliokwenda kula chakula cha mchana nyumbani waliorejea walikuwa wanne kwa ajili ya vipindi vya mchana na wengine hawakuweza kurudi nyumbani kwa chakula cha mchana kwasababu ya umbali.

Pia, amesema ratiba ya wanafunzi wa shule za msingi kuwa na saa nyingi zaidi ya ile ya shule ya sekondari ambapo kwa sekondari ratiba ya masomo huisha saa 8.30 mchana wakati ya msingi humalizika saa 9.30 mchana.

Ofisa wa Elimu Mkoa wa Dodoma, Maria Lyimo amesema wanafunzi 12,052 sawa na asilimia 22.23 walishindwa kumaliza darasa la saba mwaka 2017 kwa sababu ya utoro huku mwaka 2016 wakishindwa kumaliza 12,406 sawana asilimia 24.95.


SABABU YA WANAFUNZI KUFANYA VIBAYA KATIKA ELIMU DODOMA NI WAZAZI SABABU YA WANAFUNZI KUFANYA VIBAYA KATIKA ELIMU DODOMA NI WAZAZI Reviewed by KUSAGANEWS on February 20, 2018 Rating: 5

No comments: