Majaliwa Amtaka mkurugenzi kutoa jibu la papo hapo kuhusu mgogoro

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amempa wakati mgumu Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilemela, John Wanga baada ya kumtaka atoe jibu la papo hapo kuhusu lini wakazi wa eneo la Mhonze wilayani Ilemela watalipwa fidia ya ardhi yao waliyozuiwa kuiendeleza.
Hatua hiyo ya Waziri Mkuu imetokana na kitendo cha wakazi wa eneo hilo kumpokea kwa mabango wakilalamikia kutolipwa fidia kwa muda mrefu licha ya ardhi yao kufanyiwa tathmini na Manispaa ya Ilemela wakitakiwa kuhama kwa ajili ya usalama wa Uwanja wa Ndege Mwanza
"Kama tayari tathmini imefanyika na wananchi kuzuiwa kuendeleza maeneo yao, kwanini hamuwalipi fidia ili waondoke? Mkurugenzi nataka majibu ya kueleweka hapa hapa,” Waziri Mkuu akadai majibu kutoka kwa Wanga
Bila kutaja lini wananchi hao watalipwa fidia, Wanga (huku wananchi wakiguna), akasema malipo yamecheleweshwa na kitendo cha baadhi ya wakazi wa eneo hilo kuendeleza maeneo yao baada ya zoezi la tathmini
“Sitaki majibu ya kuzungukazunguka; je, fedha za kulipa fidia zipo na ni lini wananchi hawa watalipwa?” akasisitiza swali Waziri Mkuu na kuibua shangwe kutoka kwa wananchi
Swali hilo likaonekana gumu kwa Wanga na kuomba msaada kwa ofisa ardhi (jina halikujulikana mara moja), ambaye pia akalikwepa kwa kusema ana muda mfupi tangu alipoanza kazi Manispaa ya Ilemela, hivyo hawezi kujua iwapo fedha zipo hadi apitie nyaraka.
Mkuu wa mkoa wa Mwanza, John Mongella amelazimika kuingilia kati kuokoa jahazi kwa kuahidi kuwa suala hilo litashughulikiwa na kumalizika ndani ya kipindi cha miezi mitatu, jibu lililomridhisha Waziri Mkuu
“Angalau kidogo maelezo ya mkuu wa mkoa nayaelewa; kwa hiyo wananchi tusubiri huo muda alioahidi mkuu wa mkoa,” Majaliwa akawaeleza wananchi waliolipuka kwa shangwe
Akizungumzia kero na migogoro ya ardhi nchini, Waziri Mkuu amesema nyingi ni matokeo ya watendaji wa halmashauri kutumia muda mwingi kukaa maofisini badala ya kwenda kwa wananchi kusikiliza na kutatua kero zao

“Nimeshaagiza maofisa ardhi wote nchini waende kwa wananchi kusikiliza na kutatua matatizo na kero za ardhi; utatuzi wa kero na migogoro ya ardhi itakuwa miongoni mwa vigezo vya kupima utendaji na uwajibikaji,” amesema Majaliwa.


Majaliwa Amtaka mkurugenzi kutoa jibu la papo hapo kuhusu mgogoro Majaliwa Amtaka mkurugenzi kutoa jibu la papo hapo kuhusu mgogoro Reviewed by KUSAGANEWS on February 21, 2018 Rating: 5

No comments: