Rais Magufuli akutana na Jaji Mkuu wa Tanzania Dodoma



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amekutana na kufanya mazungumzo na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma katika Ikulu ya Chamwino Mkoani Dodoma.

Baada ya mazungumzo hayo Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amesema Mhe. Rais Magufuli amemuahidi kuwa Serikali itatoa eneo kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama Kuu Mkoani Dodoma na kwamba ujenzi wa majengo utaanza mwezi ujao.

Ameongeza kuwa ujenzi huo utakuwa ni wa Makao Makuu ya Mahakama na Mahakama ya Rufani, na pia utaambatana na ujenzi wa makazi ya Majaji.

Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ameongeza kuwa pamoja na kuanza kwa ujenzi huo Mkoani Dodoma Mahakama inaendelea na ujenzi wa majengo ya Mahakama Kuu katika Mikoa ya Mara, Kigoma, Morogoro na Singida.

Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa ushirikiano wake kwa Mahakama na ameahidi kuwa Mahakama itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa weledi na ufanisi zaidi ikiwemo kupunguza msongamano wa mashauri mahakamani.

Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Chamwino, Dodoma
07 Desemba, 2017

Rais Magufuli akutana na Jaji Mkuu wa Tanzania Dodoma Rais Magufuli akutana na Jaji Mkuu wa Tanzania Dodoma Reviewed by KUSAGANEWS on December 07, 2017 Rating: 5

No comments: