BENKI WANACHAMA WA ATM ZA UMOJA WAKUTANA KUJADILI NAMNA YA KUBORESHA MFUMO HUO.


Na  NAMNYAK KIVUYO, ARUSHA.

Muunganiko wa benki 20 maarufu kama umoja switch wenye jumla ya mashine za ATM 270 nchi nzima wamekutana jiji Arusha kujadili  namna gani wataweza kuboresha zaidi huduma hiyo ili kuwawezesha wananchi wengi zaidi kupata malipo kupitia mfumo wa ATM.

Akiongea na waandishi wa habari katika kongamano hilo makamu mwenyekiti wa muunganiko huo Godfrey Ndalahwa  ambaye pia ni mkurugenzi mtendaji wa benki ya biashara ya DCB alisema  wana ATM za umoja ambazo zimesambaa nchi nzima kwaajili ya kuwasaidia wateja wa mabenki wananchama kuweza  kupata fedha zao kupitia njia ya ATM ambapo wamekutana kujadili mstakabali, mafanikio na namna watakavyoboresha wanakokwenda.

“Tumekutana hapa tunajadili mada mbalimbali na nyingi zinalenga katika kurahisisha mfumo wa malipo ili mteje aweze kunufaika zaidi na tunajua mfumo unaotumika sana ni huu wa ATM lakini pia tuna mifumo mingine ikiwemo wakala na simu na tunachoangali ni hii mifumo tutawezaje kuiboresha zaidi hasa kwa upande wa gharama ili wateja waweze kupata huduma kwa gharama nafuu, ” Alisema Ndalahwa.

Alieleza kuwa kwasababu malipo yanasaidiwa na mfumo wa teknolojia hivyo  pia mazungumzo yao yatalenga namna gani watatumia teknolojia kuboresha ili mlaji wa mwisho aweze kunufaika zaidi ambapo alisema kuwa wamepata  mafanikio makubwa tangu kuanzishwa kwa mashine za malipo za umoja  kwani benki nyingi ambazo zilikuwa zinapatikana eneo moja sasa kupitia umoja huo huduma zimeweza kusambaa nchi nzima.

Alifafanua kuwa pia wameanza kuungana kupitia mawakala wa mabenki wananchama wa umoja huo ambapo wateja wataanza kupata huduma za malipo kupitia mawakala wa wanachama wa umoja na tayari  benki wananchama wameshaanza kutumia VISA ambayo inamwezesha mtu kupata huduma  hata akiwa nje ya nchi.

Aidha alieleza ni kitu muhimu na kipaumbele kuhakikisha kwamba  pesa za wateja wao ziko salama ambapo katika majadiliano yao pia watajadiki masuala ya uhalifu unaweza kufanyika kupitia mifumo hiyo hivyo wananchi waendelee kutumia mashine za umoja kwani ni salama.

Kwa upande wake mkurugenzi mtendaji wa Umoja switch  Miriam Malima alisema kuwa lengo la umoja  ni kuweza kuzifikia benki ndogo hadi kubwa na kuweza kupata huduma kwa bei nafuu ili waweze kuwafikia watanzania wote wakiwemo wa vijijini.

“kwasasa tuna ATM 270 nchi nzima ambazo benki wanachama wa umoja switch wanaweza kupata huduma lakini pia tuna huduma ya miamala ya mobile banking na huduma ya mawakala wa mabenki ambapo umoja tunafanya kazi kwa kushirikiana na kwasasa tuna wanachama 20 ambazo 18 ni mabenki na 2 ni saccos,” Alisema Bi Malima.

Naye mmoja wa wadau wa mifumo hiyo Profesa Edson Lubua alisema kuwa huduma zinazotolewa na umoja switch ni muhimu sana kwao kwani  zinawawezesha kupata huduma bora kwa urahisi hivyo waendelee kupambana ili huduma hizo ziweze kuwafikia zaidi wananchi popote walipo.

“Tamaa yetu  wananchi  ni tupate huduma kwa gharama ambazo ni nafuu ambapo wakiliangalia hili itakuwa ni vema zaidi kwetu lakini pia wazidishe kuweka ATM hizo katika maeneo yote ya nchi,” Alisema Profesa Lubua.

BENKI WANACHAMA WA ATM ZA UMOJA WAKUTANA KUJADILI NAMNA YA KUBORESHA MFUMO HUO. BENKI WANACHAMA WA ATM ZA UMOJA WAKUTANA KUJADILI NAMNA YA KUBORESHA MFUMO HUO. Reviewed by KUSAGANEWS on January 27, 2022 Rating: 5

No comments: