MOTISHA YA IGP KWA ASKARI YAMUIBUA GIDABUDAY

skari Polisi wa kike WP Edith Msafiri ambaye alikuwa ni mmoja wa washiriki wa mchezo wa Taekwondo katika mashindano ya majeshi ya Polisi (EAPCCO)  akipewa mkono wa hongera toka kwa Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai mkoa wa Arusha Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP) George Katabazi katika hafla ya kuwapongeza wanamichezo hao iliyofanyika jijini Arusha (Picha na Rashid Nchimbi wa Polisi Arusha)

Mnadhimu wa Jeshi la Polisi mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Yusuf Ilembo ambaye alikuwa mgeni rasmi akiongea na wanamichezo wa Michezo ya Riadha na Taekwondo katika hafla iliyofanyika jana usiku ukumbi wa Bwalo la Maofisa wa Polisi uliopo jijini hapa. (Picha na Rashid Nchimbi wa Polisi Arusha)
Katibu wa Mkuu wa Shirikisho la Riadha nchini Bw. Wilhelmi Gidabuday akitoa pongezi zake kwa Jeshi la Polisi mkoani Arusha baada ya kuonyesha nia ya kuwajali askari wanamichezo katika hafla iliyofanyika jana usiku katika ukumbi wa Bwalo la Maofisa wa Polisi uliopo jijini hapa. (Picha na Rashid Nchimbi wa Polisi Arusha)


 Na Rashid Nchimbi
Kitendo cha Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini IGP Simon Sirro kumpandisha Cheo askari Polisi Fabian Nelson kutoka Konstebo hadi Koplo baada ya kuibuka mshindi wa mbio za mita 5,000 katika mashindano ya EAPCCO yaliyomalizika hivi karibuni jijini Dar es salaam kimetoa faraja kubwa kwa Shirikisho la Riadha nchini.

Akiongea katika hafla ya kuwapongeza askari Polisi ambao walishiriki michezo ya Riadha na Taekwondo iliyoandaliwa na Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi Ramadhani Ng’anzi  katika ukumbi wa Bwalo la Maofisa uliopo jijini hapa, Katibu wa Shirikisho la Riadha nchini Bw.Wilhelmi Gidabuday alisema kwamba anampongeza sana Mkuu wa Jeshi hilo nchini pamoja na Jeshi hilo kwa ujumla kwa uamuzi walioufanya.

Alisema kwamba kitendo hicho kimeonyesha Jeshi hilo linatambua na kuthamini mchango wa askari wake ambao wanaliwakilisha Taifa katika mashindano mbalimbali ya kimataifa hali ambayo itaendeleza hamasa.

“Kwa niaba ya Rais wa Shirikisho la Riadha nchini Mheshimiwa Anthony Mataka nichukue nafasi hii kumpongeza Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini baada ya kutoa motisha kwa kijana wake (Askari Polisi) kwa kumpandisha cheo hali ambayo imetufariji sana na ni tafsiri sahihi kwamba ili kuiletea sifa nchi yetu katika michezo yatupasa tushirikiane”. Alisema Gidabuday

Aliahidi Shirikisho hilo kuendeleza ushirikiano kwa Jeshi hilo kwa kipindi chochote ambacho watakuwa katika mashindano ya Riadha na kuliomba Jeshi hilo kuendelea kutoa nafasi za ajira kwa wanamichezo ili waweze kuendelea kuliletea sifa Jeshi hilo na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Mnadhimu wa Jeshi la Polisi mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Yusuf Ilembo ambaye  alimwakilisha Kamanda wa Polisi, alisema kwamba Jeshi hilo liliandaa hafla hiyo kama njia mojawapo ya kuwapongeza na kuwahamasisha askari  wanamichezo ili waendelee kufanya vizuri katika mashindano mbalimbali.

Aliwataka wanamichezo hao kutobweteka na ushindi walioupata badala yake wanatakiwa kuongeza juhudi ili waweze kupata mafanikio zaidi na kuahidi kuendelea kuwaunga mkono kwa hali na mali ili waweze kufanya vizuri katika mashindano mengine.

Mwanariadha Fabiani Nelson alitumia dakika 13:45:99 na kuvunja rekodi iliyowekwa na mshindi wa mwaka jana katika mashindano hayo yaliyofanyika kwa mara ya kwanza Kampala nchini Uganda ambapo askari Polisi wa Uganda Stephen Diott alishinda baada ya kutumia dakika 14:02:11.

Mashindano ya shirikisho la Majeshi ya Polisi Ukanda wa Afrika Mashariki na kati yalifunguliwa rasmi tarehe 06 Agosti mwaka huu ambapo mgeni rasmi alikuwa Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa na kufungwa tarehe 12 Agosti ambapo Tanzania ilishika nafasi ya pili katika ushindi wa jumla ambapo nafasi ya kwanza ilichukuliwa na Kenya na Uganda ilishika nafasi ya Tatu.





MOTISHA YA IGP KWA ASKARI YAMUIBUA GIDABUDAY    MOTISHA YA IGP KWA ASKARI YAMUIBUA GIDABUDAY Reviewed by KUSAGANEWS on August 24, 2018 Rating: 5

No comments: