Wahamiaji haramu wabadili Mfumo waja kimasai

Jeshi la Uhamiaji Mkoa wa Kilimanjaro, limebaini mbinu mpya wanayotumia mawakala kusafirisha wahamiaji haramu ambapo kwa sasa wanawabadili mwonekano kwa kuwanyoa vipara na kuwavisha mavazi yanayotumiwa na kabila la kimasai ili kuvikwepa vyombo vya sheria.

Katika kipindi cha Januari 2017 hadi Machi 22,2018, jeshi hilo limewakamata wahamiaji haramu 208, katika maeneo mbalimbali mkoani Kilimanjaro, kwa tuhuma za kuingia nchini, kinyume cha sheria
Akizungumza ofisini kwake leo Machi 23 Mkuu wa Uhamiaji Kilimanjaro, Naibu Kamishna wa Uhamiaji Albert Rwelamira, amesema  Machi 22 mwaka huu, waliwakamata watu wawili katika mpaka wa Holili, akiwemo raia mmoja wa Ethiopia, ambaye alikuwa amevalia mavazi ya kimasai huku akiwa amenyoa upara kwa lengo la kukwepa vyombo vya ulinzi maeneo ya mpakani
Aliwataja watu waliokamatwa kuwa ni Saimon Ngarieni Kalanga (28)Masai, mkazi wa Simanjiro mkoani Manyara, ambaye alikuwa akimsafirisha Kibamo Gashe Abate (26) Raia wa Ethiopia, kwenda nchini Afrika Kusini
“Katika kupambana na wahamiaji haramu, tuna mitandao tunayoifuatilia, na tumebaini njia wanazozitumia ili kutukwepa kwani awali walikuwa wakipita vichochoroni, lakini kwa sasa wanawabadilisha muonekano, wanawanyoa nywele zote na kubaki upara na kuwavisha mavazi ya kimasai (rubega) ili kutukwepa,” amesema Rwelamira
Amesema  Mtanzania ambaye alikuwa akimsafirisha raia huyo wa Ethiopia, mbali na kumbadilisha muonekano, pia alimbadilisha jina na kumpa majina ya Samuel  ili kumficha katika basi walilokuwa wakisafiria asifahamike kiurahisi
Kwa mujibu wa Kamishna Rwelamira raia huyo wa Ethiopia, alikuwa na hati ya kusafiria namba Ep 50554339, ambayo inaonyesha kutolewa Februari 22 mwaka huu nchini Ethiopia na alitoka nchini humo Machi Mosi mwaka huu akipitia nchini Kenya, ambapo iligongwa muhuri lakini alipofika Tanzania hakuitumia kutokana na utaratibu wa viza uliopo ambao wanadai ni mgumu
“Tunaendelea na jitihada za kupambana na mtandao wa kusafirisha wahamiaji haramu ambao unaonekana kuwezeshwa na baadhi ya Watanzania kwani mawakala wa usafirishaji wapo kuanzia Ethiopia kwenyewe Kenya, Tanzania, Zimbabwe hadi Afrika Kusini, na hapa unaweza kuona ni kiasi gani cha fedha wanachotumia katika kazi hii.”

Pia alisema katika kupambana na hali hiyo tayari wamezungumza na wawakilishi wa kampuni za magari, kuwataka kuwa makini hasa wakati wa ukataji wa tiketi na kuhakikisha wale wanaofika kuwakatia watu ambao hawapo, wanafika na vitambulisho vyao vyenye picha ili kujiridhisha

Alisema kwa mujibu wa sheria likikamatwa gari lililobeba mhamiaji haramu linatakiwa kutaifishwa hivyo ni vyema wakawa makini na kuhakikisha wanatoa taarifa pindi anapoingia mtu kwenye gari na kumtilia shaka

“Lazima wajiulize, mtu anayekuja kukata tiketi ya watu wawili au watatu na watu hao hawapo, hivyo wahakikishe wanakuja na vitambulisho vyao vyenye picha ili kujiridhisha kama majina yanafanana, watusaidie katika hili, wasiangalie maslahi ya kibiashara, waangalie maslahi ya taifa na usalama wa nchi”
Wahamiaji haramu wabadili Mfumo waja kimasai Wahamiaji haramu wabadili Mfumo waja kimasai Reviewed by KUSAGANEWS on March 23, 2018 Rating: 5

No comments: