Hukumu ya Babu Seya, Papii Kocha kusomwa kesho

Mahakama ya Afrika na Haki za Binadamu (AfCHPR) kesho Ijumaa Machi 23, 2018 itasoma hukumu ya kesi ya wanamuziki wa dansi, Nguza Viking maarufu Babu Seya na mwanaye, Johnson Nguza ‘Papii Kocha’

Wanamuziki hao walikata rufaa iliyosajiliwa na kupewa namba 006/2015 katika mahakama hiyo kupinga kifungo cha maisha.

Wakati hukumu hiyo ikitarajiwa kusomwa kesho, Babu Seya ambaye ni mtunzi wa kibao maarufu cha “Seya” na Papii Kocha ambaye wameshirikiana katika wimbo huo ni miongoni mwa wafungwa 8,157 waliosamehewa na Rais John Magufuli siku ya Uhuru wa Tanganyika, Desemba 9, 2017

Walikuwa kati ya wafungwa 61 waliokuwa na adhabu za vifungo vya maisha na kunyongwa ambazo si rahisi kupata msahama wa kawaida wa mkuu wa nchi unaotolewa siku ya sherehe hizo

Rais wa mahakama hiyo, Jaji Sylvian Ore alisema itasoma hukumu hiyo baada ya kukamilisha mahitaji yote na kupata taarifa za wakata rufaa

Hata hivyo, wakati Jaji Ore akiahirisha kusoma hukumu hiyo, wanamuziki hao hawakuwepo mahakamani

Baadhi ya mawakili waliokuwepo mahakamani hapo wamesema licha ya kuwa wanamuziki hao wamepata msamaha wa rais, hukumu yao itasomwa

"Mahakama hapa itatoa hukumu ili kuweka rekodi za kimahakama katika kesi za aina hii na hata kama ikieleza walikuwa na hatia haina athari kwao,” amesema wakili Daniel Kalasha

Katika kesi hiyo, Jamhuri inawakilishwa na mawakili Sara Mwaipopo na Nkasori Sarakikya.
Hukumu ya Babu Seya, Papii Kocha kusomwa kesho Hukumu ya Babu Seya, Papii Kocha kusomwa kesho Reviewed by KUSAGANEWS on March 22, 2018 Rating: 5

No comments: