GODWIN GONDWE ATATUA MGOGORO

Mgogoro baina ya wakazi wa Kijiji cha Mapangoni wilayani hapa na Jeshi la Magereza umeingia katika sura nyingine baada ya Serikali kuingilia kati na kukanusha uvumi ulioenea kwamba askari 11 waliopo mahabusu wametoroka.

Serikali imesema askari hao wanaotuhumiwa kwa mauaji ya mkazi wa kijiji hicho, Aloyce Makala (41) wapo mahabusu wakisubiri kesi yao kusikilizwa na kutolewa hukumu na kuwataka wananchi kuacha kusikiliza maneno ya mitaani badala yake wasubiri mahakama ifanye kazi yake

Kaimu mkuu wa wilaya ya Korogwe, Godwin Gondwe alifanya ziara kijijini hapo kwa lengo la kutatua mgogoro huo ambao uliibuka baada ya kutokea mauaji hayo Januari 22 mwaka huu

Alisema kuwa askari wote 11 wanaotuhumiwa kuhusika na mauaji ya mwananchi huyo  wapo kwenye mikono ya sheria na tayari wameshafikishwa mahakamani

Aliwataka wakazi wa kijiji hicho wasiichukie taasisi ya magereza kuwepo kwenye eneo hilo kwani ipo  kwa ajili ya manufaa  yao ila wale ambao wamehusika kuharibu amani kwa wananchi wameshafikishwa kwenye vyombo vya dola

"Serikali haiangalii wadhifa wa mtu katika uwajibikaji, yeyote atakaekosea sheria itafuata mkondo wake na ikibainika amefanya makosa hatua za kisheria dhidi ya mhusika lazima zichukuliwe," alisema Gondwe.

Aliwataka wananchi wa kijiji cha Mapangoni kuhakikisha kuwa na uhusiano  mzuri na Jeshi la Magereza  kwani si wote waliohusika katika hilo suala lililotokea

Diwani wa kata ya Kelenge, Shebila Saidi alisema kutokana na tukio hilo, ni vyema kwa sasa taasisi hiyo ya magereza kuondoa kambi yao iliyopo kwenye kijiji cha Mapangoni ili kuweza kuwepo amani na ushirikiano mzuri kwani bado wapo wananchi wenye kinyongo

Alisema tukio lililotokea limeleta taswira mbaya miongoni mwa wananchi hivyo kwa muda magereza wahamishe taasisi yao irudi makao makuu ya Korogwe hadi pale vuguvugu hilo litakapopatiwa

Mmoja wa wananchi wa kijiji cha Mapangoni, Mashaka Mussa alisema mara kwa mara kumekuwepo na mahusiano yasiyoridhisha baina ya askari hao na wananchi ambapo hata yeye alishagombana na  askari magereza wawili kwa kukatiwa migomba yake shambani na alipokwenda baraza la ardhi alishinda kesi

Hata hivyo kaimu mkuu wa jeshi la polisi wilaya ya Korogwe Saidi Mwagara aliwataka wananchi wa eneo hilo kuhakikisha wanalinda amani yao kwa kukwepa vitu ambavyo vinasababisha ukosefu wa amani kwani ni rahisi kuondoa amani ila si kuirudisha

Askari wa Jeshi la Magereza waliofikishwa mahakamani hapo kwa shitaka hilo ni  Jonas Makere, Shadrack Lugendo, Razalo Stephen, Musa Zuberi, Ramadhan Yusuf, Robert Alfred, Fredrick Osmas, Alfonce Revocatus, Mbesha Naftari, Hamis Msola na Michael Elia.
GODWIN GONDWE ATATUA MGOGORO GODWIN GONDWE ATATUA MGOGORO Reviewed by KUSAGANEWS on March 23, 2018 Rating: 5

No comments: