Serikali imesema kwamba kuhamia
Dodoma haiondoi hadhi ya Jiji la Dar es Salaam, na kwamba mji huo utabaki kuwa
sehemu ya biashara.
Hayo yamesemwa leo na Waziri
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa wakati
akifungua ofisi ya Shirika la maendeleo ya Umoja wa Mataifa na
kuongeza kuwa kuwepo kwa ofisi ya Umoja wa Mataifa mkoani Dodoma ni ishara ya
kukamilika kwa serikali kuhamia rasmi mkoani humo.
"Leo nafungua ofisi ya Shirika
la Umoja wa Mataifa hapa Dodoma, zaidi ya watumishi 2376 wameshahamia Dodoma,
mimi tayari nimehamia mapema, Makamu wa Rais Samia Suluhu ataungana nasi mwishoni
mwa mwezi huu , mwakani tunategemea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
John Pombe Magufuli atahamia huku", amesema Majaliwa.
Pia ameongeza kwa kusema,
"Umoja wa Mataifa una mchango mkubwa sana katika Taifa letu, imechangia
mipango mingi ya maendeleo , mpango wa kwanza ulianza mwaka 2011, wakati huu wa
pili umeanza 2016 na utaishia 2021".
Aidha Majaliwa amesema hadhi ya mkoa
wa Dar es salaam haitopungua ila itakuwa sehemu rasmi ya biashara.
"Viongozi kuhamia Dodoma
hakuharibu hadhi ya mkoa huo, utabakia kuwa ni sehemu sahihi ya biashara,
tunatengeneza njia sita ambazo zitatoka Ubungo hadi Chalinze,
tunaimarisha mwendokasi ufike maeneo mengi pamoja na njia za reli iendayo
haraka" , ameongeza Majaliwa.
Mpango wa kuhamia Dodoma ulianzishwa
na aliyekuwa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere mwaka 1973,
utekelezaji umeanza kufanyika mwaka 2017 ndani ya uongozi wa Rais John Pombe
Magufuli.
Majaliwa aizungumzia Dar es salaam itakavyobaki Baada ya Serikali Kuhamia Dodoma
Reviewed by KUSAGANEWS
on
December 07, 2017
Rating:

No comments:
Post a Comment