CCM Arusha yawachimbia mkwara wagombea

Katibu wa CCM wilaya ya Arusha mjini, Ramadhani Dallo amesema  atawachukulia sheria wanachama wanaogombea nafasi mbalimbali ambao  watagundulika kukiuka kanuni na  sheria za uchaguzi.

Dallo ameyasema hayo leo wakati akizungumzia mchakato wa uchukuaji fomu kwa ajili ya kugombea nafasi mbalimbali ngazi ya wilaya. 

Kanuni hizo ni pamoja na kutofanya kampeni, kutangaza nia au kujinadi kwa aina yoyote.

Zoezi  la uchukuaji na urudishwaji fomu lilianza Julai 2 na litafungwa Julai 10.

 “Katika kipindi hiki cha uchukuaji fomu na urudishwaji, wanachama pamoja na wagombea hao wanapaswa kufuata sheria na kanuni zote za uchaguzi zilizowekwa na yeyote atakayekiuka atachukuliwa sheria kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa.”amesema

Hivyo aliwataka wanachama wa chama hicho pamoja na wagombea kuendelea kufuata taratibu hizo kwani  mgombea yeyote atakayegundulika kukiuka taratibu atakuwa amejiondoa wenyewe .

Dallo alizitaja nafasi zinazogombewa kuwa ni Mwenyekiti wa wilaya, Katibu Siasa na Uenezi wa Wilaya, Mjumbe wa Halmashauri Kuu wilaya nafasi 10, Mjumbe Mkutano mkuu   mkoa nafasi mbili,Mjumbe wa Mkutano mkuu Taifa nafasi tatu na Mjumbe wa Halmashauri Kuu Mkoa, nafasi mbili.

 Amesema mwamko ni mkubwa sana kwa wanachama wanaowania nafasi mbalimbali katika chama hicho.

"Kwa kweli watu wana mwamko sana wa kugombea nafasi mbalimbali na tunaendelea kuwaomba wajitokeze kwa wingi kwani kila mtu ana haki ya kuchagua na kuchaguliwa,” amesema Dallo.


CCM Arusha yawachimbia mkwara wagombea CCM Arusha yawachimbia mkwara wagombea Reviewed by KUSAGANEWS on July 09, 2017 Rating: 5

No comments: