Katibu mkuu wa zamani wa CCM, Yusuf Makamba amesema
wanaoshangaa au kuhoji hatua ya aliyekuwa mwenyekiti wa Baraza la Uongozi la
CUF, Julius Mtatiro kuhamia chama hicho tawala wanapaswa kujiuliza kama
walishangaa pia wakati mawaziri wakuu wa zamani, Edward Lowassa na Frederick
Sumaye walipohamia upinzani
Mtatiro juzi alitangaza kuachana na CUF na kuanza mchakato
wa kujiunga na CCM
Makamba aliyekuwa katibu mkuu wa CCM wakati wa utawala wa
awamu ya nne, alisema mwanasiasa kuhama chama ni utashi wake na haipaswi
kutazamwa kama jambo baya
Alisema wanaohoji wapinzani wenye ushawishi kuondoka kwenye
vyama vyao watambue pia CCM iliwahi kuwa na vigogo waliokwenda upinzani
“Kuna mtu mzito kama Lowassa? Nakuuliza kuna mtu mzito kama
Sumaye?” alihoji mwanasiasa huyo alipozungumza na Mwananchi kuhusu wimbi la
wapinzani kuvihama vyama vyao
Lowassa na Sumaye walijiondoa CCM na kujiunga Chadema kabla
ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015
Makamba alisema kama ilivyokuwa kwa Lowassa na Sumaye
walipoondoka CCM na kwenda upinzani vivyo hivyo kwa wapinzani kwenda chama
hicho tawala
Alisema kitendo kinachofanywa na wapinzani si kipya kwa kuwa
kimewahi pia kufanywa na wanasiasa wengine.
“Mbona (Augustine)
Mrema alihama CCM na kwenda kujiunga na NCCR- Mageuzi. Mbona Zuberi Mtemvu
aliondoka CCM na kwenda kuanzisha chama chake cha upinzani. Kuhama chama ni
hiari ya mtu wala sio ubaya,” alisema
Makamba alisema wanaohama chama wanavutiwa na vyama
wanavyohamia. Alisema hali inayoendelea sasa inaonyesha wanasiasa hao
wanavyovutiwa na sera za CCM.
Uongozi wa CUF upande unaomuunga mkono mwenyekiti wa chama
hicho, Profesa Ibrahim Lipumba umejitokeza kujibu hoja zilizotolewa na Mtatiro
ikiwamo mgogoro unaokikabili chama hicho
Mtatiro akitangaza kujiondoa CUF, alitoa sababu kadhaa,
ikiwamo kutaka kufanya siasa za maendeleo kwenye jukwaa sahihi na kuangalia
mustakabali wake kisiasa
Chama hicho kiliingia kwenye mgogoro mwaka 2016 wakati wa
mkutano mkuu ulioongozwa na Mtatiro kwa lengo la kujadili barua ya kujiuzulu
uenyekiti Profesa Lipumba mwaka 2015
Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Uhusiano wa Umma wa CUF,
Abdul Kambaya akizungumza na waandishi wa habari jana alidai Mtatiro amechangia
kwa zaidi ya asilimia 70 katika mgogoro ndani ya chama hicho
Kambaya alidai Mtatiro akiwa mwenyekiti wa mkutano mkuu,
alisababisha chama hicho kugawanyika kwa kutosikiliza maoni ya wajumbe na
kuamua kuuendesha kibabe ili kulinda masilahi ya upande mmoja
“Hakuna kitu ambacho Mtatiro amekifanya kwenye chama hiki,
kubwa zaidi amesababisha migogoro, ana asilimia 70 kwenye migogoro ya CUF,
hamna kitu kingine,” alidai Kambaya
Alidai Mtatiro akiwa naibu katibu mkuu alikiingiza chama
hicho kwenye mgogoro kutokana na ubadhirifu wa Sh300 milioni kwenye uchaguzi
mdogo wa Igunga.
Kambaya akizungumzia kauli ya Mtatiro kwamba aliasisi ilani
ya CUF iliyolenga kutoa elimu bure, alisema si kweli kwa sababu suala hilo
lilianza kuzungumzwa kuanzia mwaka 2000 kabla hata hajawa mwanachama
Alisema mafanikio ya CUF yametokana na jitihada za muda
mrefu hasa kwenye mikoa ya Kusini ambako walishinda majimbo saba.
“Wanasiasa
walio-strong huwa hawakimbii migogoro ndani ya vyama vyao, bali wanakaa
humohumo mpaka migogoro itakapokwisha,” alisema
Alipoulizwa kuhusu tuhuma za ubadhirifu wa fedha na kuwa
chanzo cha migogoro, Mtatiro hakutaka kuzungumzia suala hilo akisema
alishazungumza kujitoa katika chama hicho alipozungumza na waandishi wa habari
Makamba afunguka Mtatiro kuhamia CCM
Reviewed by KUSAGANEWS
on
August 12, 2018
Rating:
No comments:
Post a Comment