TAHADHARI KICHAA CHA MBWA


HOSPITALI ya rufani ya mkoa wa Kilimanjaro (Mawenzi), imetoa tahadhari kwa umma kuhusu kuwapo kwa ugonjwa wa kichaa cha mbwa ambao hadi sasa umesababisha vifo vya watu wanne katika kipindi kisichozidi siku 60.

Tahadhari hiyo ilitangazwa jana, na Ofisa afya wa hospitali hiyo, Dk. Jonas Mcharo, wakati akizungumzia mlipuko wa ugonjwa huo katika Wilaya ya Moshi.

“Kichaa cha mbwa ni ugonjwa hatari sana na virusi vya ugonjwa huo husababisha uvimbe kwenye ubongo (encephalytis). Virusi hivi vinaweza kutokea kwa binadamu na wanyama, lakini ni mara chache hutokea kwa wanyama. Mpaka sasa kuna watu watatu wamefariki kwa ugonjwa huo na mmoja alishambuliwa na paka,” alisema.

Watu hao wanadaiwa kufariki dunia wakati wakipatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufani ya KCMC, baada ya kung’atwa au kuumwa na mbwa wenye ugonjwa huo.

Kwa mujibu wa wataalamu wa afya, kwa kawaida chanjo ya kichaa cha mbwa iliyothibitishwa na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Wazee na Watoto kwa ajili ya huduma hiyo ni Anti-Rabies, ambayo awali ilikuwa ikihifadhiwa katika minyororo baridi kwenye hospitali za mkoa,

Inelezwa kuwa kichaa cha mbwa kinaweza kusambazwa kwa mate ya wanyama wakiwamo paka, popo, ng'ombe, mbweha, fisi na wengine.

Moja ya dalili za ugonjwa huo ni maji ya bomba yanapofunguliwa mgonjwa huogopa na akionyeshwa kikombe cha maji anaweza kukitupa, dalili nyingine ni kushindwa kula chakula na wakati mwingine katika hatua za mwisho mgonjwa hutoka udenda uliochanganyika na damu.
Dk. Mcharo alisema wakazi 64 wa Kijiji cha Mawala, Kata ya Kahe, Halmashauri ya Wilaya ya Moshi, wamejitokeza kwa hiari kupatiwa chanjo ya kujikinga na ugonjwa huo.

TAHADHARI KICHAA CHA MBWA TAHADHARI KICHAA CHA MBWA Reviewed by KUSAGANEWS on April 07, 2018 Rating: 5

No comments: